MWINYI Zahera, aliyekuwa Kocha Mkuu wa Yanga, ametoa hadharani siku moja baada ya kufutwa kazi katika klabu hiyo, na kudai kuwa Mwenyekiti wa Yanga, Dk. Mshindo Msolla amemgeuka. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Zahera amesema uongozi wa Yanga umemgeuka, kwa madai kwamba walimhakikishia kuwa ataendelea kuinoa klabu hiyo, hata kama itafanya vibaya katika michuano ya kimataifa.
Zahera ameeleza kuwa, Dk. Msolla alimueleza kwamba uongozi wa klabu hiyo unamuunga mkono, licha ya kwamba mashabiki na wanachama walitaka kumng’oa.
“Mwenyekiti aliniambia, Kocha hao sio wote mashabiki wa Yanga, sisi uongozi tuko pamoja na wewe, ” amesema Zahera.
Hata hivyo, Zahera amesema Mwenyekiti huyo alimdokeza kwamba, kuna baadhi ya viongozi wa Yanga walitaka kumng’oa, lakini harakati zao ziligonga mwamba kutokana na hoja zao kukosa mashiko.
Zahera amesema: “Mwenyekiti (Dk. Msolla) alinimbia kuwa aliambiwa na Ndama kwanini wasinifukuze, lakini Mwenyekiti akamwambia atoe sababu za kuniondoa. Alimwambia kufungwa na Pyramids ni ajabu kubwa? Hakuna mtu atashangaa, akamjibu sisi tumuonde kocha kwa sababu gani?”
Kocha huto Mkongo ameeleza kuwa, Mwenyekiti alimshauri kuwahimiza wachezaji kujituma uwanjani, kwani timu ikifanya vizuri wanachama na mashabiki hawatasema.
Leave a comment