MENEJA wa mradi wa kuleta maeuzi katika Sekta ya mkaa Tanzania (TTCS), Leonard Charles ameishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuamua kuunda kikosi kazi cha kuangalia namna ya kupitisha Sera ya mkaa itakayosaidia kuboresha uhifadhi misitu unaoendana na mabadiliko ya tabia nchi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Hayo yalisemwa jana na Meneja wa TTCS, Charles wakati akizungumza na maofisa mbalimbali kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Serikali Kuu waliokutana mkoani Morogoro.
Charles alisema, Sera ya mkaa ambayo haikuwepo tangu zamani huku wakitumia ya misitu kuundwa kwake kutasaidia vijiji kuendeleza uvunaji mkaa kwa njia endelevu inayoleta manufaa kwenye vijiji na hata Halmashauri.
“Tunaishukuru Serikali kwa kuunda kikosi kazi cha kuangalia sekta ya mkaa, huku kikiangalia namna ya uwepo wa sera ya mkaa Tanzania, hii itasaidia kuboresha zaidi mfumo wa uvunaji mkaa kwa njia endelevu,” alisema.
Alisema, ipo haja kama serikali kukuza na kuendeleza mradi huo kwani mradi unalengo la kuleta mabadiliko kwenye mnyororo wa thamani ambayo yatasaidia kukuza kipato na hata kuboresha misitu kwa lengo la kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Naye Ofisa Msaidizi misitu kutoka wilaya ya Songea, Hadija Shemhina alisema, mfumo huo wa mradi wa mkaa endelevu ni mzuri kutumika pia katika maeneo mengine ili kupunguza hali ya uharibifu wa misitu unaofanywa na wakataji mkaa kiholela na wavunaji wengine wa misitu kiholela.
Leave a comment