WATU wanaosumbuliwa na magonjwa sugu pamoja na unene uliopitiliza wako hatarini kupoteza maisha, kutokana na Ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa jana tarehe 9 Aprili 2020 na Dk. Faustine Ndugulile, Naibu Waziri wa Afya, kupitia ukurasa wake wa Twitter.
Dk. Ndugulile ameeleza kuwa, magonjwa hayo sugu ni pamoja na kisukari, shinikizo la damu, pumu na ugonjwa wa moyo.
Kufuatia tishio hilo, Dk. Ndugulile amewataka wahusika kupima afya zao pamoja na kuzingatia ushauri unaotolewa na watalaamu wa afya.
“Mtu mwenye magonjwa sugu kama kisukari, shinikizo la damu, pumu, ugonjwa wa moyo na unene uliopitiliza huathirika zaidi na Covid-19 na huweza kupoteza maisha. Tupime afya zetu na kuzingatia ushauri wa kitaalamu juu ya magonjwa haya,” ameandika Dk. Ndugulile.
Mtu mwenye magonjwa sugu kama kisukari, shinikizo la damu, pumu, ugonjwa wa moyo na unene uliopitiliza huathirika zaidi na Covid-19 na huweza kupoteza maisha. Tupime afya zetu na kuzingatia ushauri wa kitaalamu juu ya magonjwa haya. #COVID19Tanzania #Covid19TZA #Covid19TZ
— Faustine Ndugulile (@DocFaustine) April 8, 2020
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, juzi tarehe 8 Aprili 2020, kwa sasa Tanzania ina wagonjwa 25 wa COVID-19, tangu ugonjwa huo ulipuke nchini.
Jana , Waziri Ummy wakati akifungua kikao cha watalaamu wa afya na viongozi wa dini, aliwahimiza viongozi hao kuchukua tahadhari katika sehemu za ibada, hasa katika kipindi hiki cha msimu wa Siku Kuu ya Pasaka kwa waumini wa Kikristo. Kwa kufanya ibada za muda mfupi na kuepuka msongamano wa watu wengi.
Pia, Waziri Ummy aliwataka viongozi wa dini ya kislamu kuhakikisha maeneo ya ibada yanafanyiwa usafi kila mara na kupulizia dawa za kuwa Virusi vya Corona, hasa katika maeneo ambayo waumini wake wanatumia kuswali.
Leave a comment