SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano inamuandalia Mansour Yussuf Himid mashitaka ambayo akishasomewa mbele ya mahakama atapelekwa gerezani. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mansour aliyekuwa waziri na mjumbe wa halmashauri kuu ya taifa ya CCM alifukuzwa chama hicho na kujiunga na Chama cha Wananchi (CUF) na kuwa msaidizi wa karibu wa Maalim Seif Shariff Hamad kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, 2015.
Jeshi la Polisi hapa lilimuita Mansour siku ya Jumatano Januari 2 na kumshikilia kwa saa kadhaa kabla ya kumuachia kwa dhamana yake mwenyewe na mdhamini mmoja.
Taarifa zinasema kuwa Mansour huenda atashitakiwa kwa makosa ya uhaini ambayo yatamlazimu kukosa dhamana. Uhaini ni miongoni mwa makosa yasiyompa dhamana mshitakiwa kwa mujibu wa sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Akiwa kituo kikuu cha polisi Madema cha Mkoa wa Mjini Magharibi, Mansour alielezwa tuhuma kuwa anakusanya fedha zipatazo Sh. 30 milioni ili kufadhili mpango wa kuitoa serikali inayoongozwa na Dk. Ali Mohamed Shein.
Kwenye ukurasa wake wa Twitter aliandika juzi mara baada ya kuachiwa kuwa Polisi ilimueleza kuwa anakusudia kuajiri wanamgambo wa Kisomali katika kutekeleza “mpango huo.”
Jana@tanpol wamenishutumu kukushanya Mill 30 kwa wafanyabiashara Pemba za kuingiza silaha na wasomali Nchini ili kuipindua Serikali na kwamba tayari nishafanya vikao kadhaa na wasomali hao hapa Zbar..nimewaambia walilolidhamiria WALIFANYE Allah ni muweza ya kila jambo#ubayatu
— mansoor himid (@mansoorhimid) January 3, 2019
Polisi walimfahamisha kuwa amekusanya fedha kwa wafanyabiasharambalimbali na amepanga kuingiza nchini silaha pamoja na “askari” wa Kisomali. Tayari ameendesha vikao kadhaa kuhusu mpango wanaomtuhumu.
“Niliwaambia tekelezeni hilo mlilolidhamira dhidi yangu; Mungu yuko anajua kila kitu,” aliandika kwenye akaunti yake ikiwa ni majibu yake kwa Polisi baada ya kumuarifu anachotuhumiwa.
Kwa upande wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi wamekuwa wakirushiana mpira kutoa ufafanuzi juu ya kukamatwa na kuachiwa kwa Mansour pamoja kuwepo kwa mpango wa kusukiwa kesi ya uhaini.
Mwandishi wa Habari hizi alipiga simu kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Kamanda Thobias Sedoyeko,m alisema hawezi kulizungumzia suala hilo kwa kuwa Mansour aliitwa na Naibu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (D-DCI) Zanzibar Maulid Mabakila.
“Siwezi kukwambia chochote kwa kuwa mimi sikumuita Mansour. Mtafute Naibu Mkurugenzi wa makosa ya Jinai (D-DCI Maulidi Mabakila) yeye ndiye atakayekueleza kila kitu,” alisema RPC Sedoyeko.
Mwandishi alipomtafuta D-DCI, Mabakila, jana tarehe 4 Januari, 2019 majira ya saa 11 jioni, alisema mwenye nafasi ya kulizungumzia hilo ni Mkuu wa upelelezi wa Mkoa wa Mjini Magharibi (RCO) Kheri kwa ufafanuzi zaidi.
RCO Kheri alipopigiwa simu muda mchache baada ya mwandishi kumaliza kuzungumza na (D-DCI), alisema kuwa yeye ni mpelelezi hivo tumtafute Mkuu wa Polisi wa Mkoa wa mjini Magharibi, ambaye awali alisema hawezi kuzungumzia sakata hilo.
Mansour aliwahi kutungiwa kesi na Polisi ya kuongoza mpango wa kulipua maskani ya Kisonge ya CCM baada ya uchaguzi mkuu lakini hakupata kufikishwa mahakamani.
Mansour ambaye ni mwanafamilia katika familia ya Rais mstaafu Amani Abeid Karume, aliwahi kufunguliwa mashitaka ya kukutwa na kumiliki silaha isivyo halali. Alipata dhamana lakini kesi haijasikilizwa.
Mansour alionesha uzalendo wa Kizanzibari tangu akiwa serikalini wakati wa uongozi wa Dk. Shein katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyoishi Novemba 2010 mpaka Oktoba 2015. Alikuwa akitoa kauli za kuitetea Zanzibar na anajulikana kwa umaarufu kwa kauli yake kuwa “Tuachiwe tupumue” akimaanisha Wazanzibari waachiwe wasibanwe kiuchumi na kisiasa kwa sera za Muungano.
Alipoonekana amezidi msimamo aliandaliwa kikao cha viongozi wa juu wa CCM ambako aliambiwa amevuliwa uanachama.
Tangu hapo alianza harakati za kusaidia CUF na kuteuliwa Katibu wa mkakati wa kumpeleka Maalim Seif madarakani.
Katika harakati hizo alishirikiana pia na Mohamed Riyami (Eddi Riyami), kada mwingine aliyehamia CUF kama hatua ya kumuunga mkono Mansour kwa kusema alionewa na CCM bila ya kujali mchango kwa chama hicho.
Mansour ametakiwa kurudi Polisi mapema wiki ijayo.
Leave a comment