DAKTARI Hamisi Kigwangalla, Waziri wa Maliasili na Utalii ameonesha hofu ya kuuawa, akidai kuwepo kikundi cha watu wanaopanga kutekeleza njama hizo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, kikundi hicho kinapanga njama hizo, kwa kuwa amekuwa kikwazo katika mikakati yao ya ujangili na ufisadi wa fedha za serikali, kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii.
“Ukiwa Waziri wa Maliasili na Utalii ukakuza idadi ya watalii kwa kasi, ukaongeza mchango wa sekta yako kwenye pato la Taifa, ukadhibiti ujangili, ukaufanya utalii kuwa ‘fashionable’, badala ya kupendwa unashambuliwa, ukijiziulu ni kuwapa ruhusa kuendelea na mambo yao,” ameeleza Dk. Kigwangalla kupitia ukurasa wake wa Instagramu.
Waziri huyo amedai kuwa, watu wasiomtakia mema walijaribu kumuuawa kwa kumtengenezea ajali, lakini jaribio hilo lilishindwa, kwa kuwa serikali ilimuwekea ulinzi wa kutosha.
“Kwa wanaokumbuka wakati nimelazwa ICU na kisha wodini, ilikuwa ngumu kunitembelea na kuniona, paliwekwa ulinzi mkali sana. Watu wote walizuiliwa kuingia isipokuwa kwa kibali cha Ikulu, hadi mawaziri wenzangu hawakuruhusiwa, nilishangaa sana ila niliambiwa ndiyo hivyo,” amesema Dk. Kigwnagalla na kuongeza:
“Baadaye nikaja kujua kuwa, kuna watu walipanga njama za kuniua na hiyo ingeweza kuwa fursa kwao kunimalizia (ndio maana paliwekwa ulinzi mkali Hospitali), baada ya kuteuliwa tu, wizara hii kulizuka mtafaruku mkubwa sana juu ya usalama wangu, nilifuatiliwa kila kona.”
Kauli hiyo ya Dk. Kigwangalla imekuja siku kadhaa baada ya gazeti moja la wiki nchini, kumtuhumu kwamba, anafanya ufisadi katika wizara yake.
Dk. Kigwangalla amekanusha madai hayo ya ufisadi akisema, kwamba ni muendelezo wa mikakati ya maadui zake, wanaotaka kumng’oa katika wizara hiyo.
“Wakaona wafanye mwendelezo kupitia gazeti, sijataka kujibishana nalo, tutakutana mahakamani ambapo mbivu na mbichi zitajulikana, ukweli utawekwa wazi na rekodi itakaa sawa, sijashangaa kuwa wahusika ni wale wale wa kipindi kilichopita,hakuna jipya,” ameeleza Dk. Kigwnagalla.
Amesema, uadui huo umeibuka kwa kuwa anawakwamisha watu hao kutekeleza mikakati yao ya kutafuna fedha za serikali.
“Sababu ni deal yao binafsi, ambayo haitekelezeki bila ridhaa ya Waziri, na bahati mbaya kwao Waziri ni mimi, walitamani nisiwepo watafune pesa za Serikali vizuri, wamekwama, tutaendelea kudhibiti kimyakimya,” amesema Dk. Kigwangalla.
Hata hivyo, Dk. Kigwangalla amesema vita hiyo iliyoibuka haitamkatisha tamaa na ataendelea kutekeleza majukumu yake ya kuijenga nchi.
Leave a comment