UMMY Mwalimu, Waziri wa Afya, amewataka Watanzania kuwalinda watoto na wazee dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na virusi vya corona (Covid-19). Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Waziri Ummy ametoa wito huo leo Ijumaa tarehe 15 Mei, 2020 jijini Dar es Salaam, wakati akizungumza kuhusu Siku ya Familia Duniani ambayo huadhimishwa tarehe 15 Mei, kila mwaka.
Tangu tarehe 17 Machi 2020, wanafunzi wako nyumbani kufuatia agizo la Serikali la kufunga shule na vyuo, ili kupunguza maambukizi ya Covid-19.
Agizo la kufungwa kwa shule na vyuo lilitolewa na Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Tanzania, ambapo alisema shule hizo zitaendelea kufungwa, hadi pale Serikali itakapotoa taarifa nyingine kuhusu agizo hilo.
Kufuatia agizo hilo, Waziri Ummy amewataka wazazi na walezi kuwa karibu na watoto, pamoja na kuwaandalia mazingira bora ya kusoma wakiwa nyumbani, ili waepuke kuzurura mitaani, hali inayoweza sababisha waambukizwe Covid-19.
Waziri Ummy amewataka walezi na wazazi kufuatilia hali za watoto na wazee, na kwamba kama hali zao za afya zitakuwa na mabadiliko, hasa kuhusiana na dalili za Covid-19, watoe taarifa katika mamlaka husika.
“Niwaombe wazazi na walezi muwe karibu na familia zenu, hasa watoto na wazee na punde mnapobaini dalili za ugonjwa wa corona, watoe taarifa ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa,” amesema Waziri Ummy.
Wakati huo huo, Waziri Ummy amezitaka familia kutowanyanyapaa watu walioambukizwa ugonjwa wa Covid-19, bali wachukua hatua stahiki katika kuwalinda wasioambukizwa, pamoja na kuhakikisha walioambukizwa wanapata matibabu.
“Familia ni msingi wa ustawi wa jamii yoyote ile hivyo ni muhimu kuilinda ili kufikia maendeleo endelevu na kuhakikisha tunailinda na maambukizi ya virusi vya corona,” amesema
Akizungumzia kuhusu maadhimisho ya siku ya familia, Waziri Ummy amewataka wazazi na walezi kuziongoza vyema familia zao, dhidi ya mapambano ya kudhibiti ugonjwa wa Covid-19.
Pia, amewataka Watanzania kuendelea kufuata kanuni na maelekezo ya wataalamu wa afya ili kujikinga na kuwakinga wengine dhidi ya maambukizi ya COVID-19.
Waziri Ummy amewataka Watanzania kujiepusha na mikusanyiko, kunawa mikono kwa kutumia sabuni na maji tiririka, kutumia vitakasa mikono, kuzingatia umbali wa mita moja pamoja na kuvaa barakoa.
Leave a comment