MBUNGE wa Monduli (CHADEMA), Julius Karanga, ametuhumu serikali kuwanyonya wafugaji nchini na kusema, “wakati wengine (Chama Cha Mapinduzi), wakifikiri mifugo ni chakula, wao (Chadema), wanaiona mifugo kuwa ni uchumi.” Anaripoti Mwandishi Wetu kutoka Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni wakati wa kuchangia mjadala wa bajeti ya wizara ya Uvuvi na Mifugo bungeni leo Alhamisi, Kalanga alisema, kwa miaka mitatu mfululizo sasa, serikali haijaweza kupeleka kwenye wizara hii, hata shilingi ya fedha maendeleo.
Alisema, “ndani ya kipindi cha miaka mitatu, serikali haijapeleka hata shilingi kwenye miradi ya maendeleo kupitia wizara hii. Ndani ya miaka mitatu, hakuna miradi yoyote ya maendeleo iliyotekelezwa kwenye wizara ya uvuvi na mifugo.”
Akaongeza: “Kinachoonekana kwenye bajeti, ni mbio za serikali za kutokomeza wafugaji, kuuwa viwanda vya ndani na kutumia mabilioni ya shilingi kuagiza bidhaa za nyama na samaki nje ya nchi.”
Kwa mujibu wa Kalanga, serikali inapoteza kiasi cha Sh. 120 bilioni kila mwaka kwa kuagiza maziwa; Sh.34 bilioni kwenye ngozi na huagiza takribani tani 4000 (elfu nne) za nyama kila mwaka.
Mapema waziri wa wizara hiyo, Luhaga Mpina aliliambia Bunge kuwa wizara yake imejipanga kutatua matatizo ya wafugaji na kuzipatia ufumbuzi changamoto za kilimo.
Leave a comment