DAKTARI Harrison Mwakyembe, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesema kuanzia msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania, kila timu itawatumia wachezaji watano tu katika mchezo mmoja. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Dk. Mwakyembe amesema hayo wakati akizungumza katika harambee kubwa ya kuichangia Klabu ya Yanga, iliyofanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam.
Amesema kuanzia msimu ujao timu hata ikisajiri wachezaji zaidi ya watano lakini itaruhusiwa kuwatumia idadi hiyo ili kutoa nafasi ya wachezaji wa ndani kupata nafasi ya kucheza.
“Hata usajiri 100 kutoka nje watakaoruhusiwa kwa mchezo mmoja watakuwa watano lengo ni kulea vipaji vya ndani,” amesema Dk. Mwakyembe.
Pia Dk. Mwakyembe amesema kanuni nyingine ambayo itazingatiwa ni kila timu inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara kuwa na timu ya Vijana chini ya umri wa miaka 20, kinyume na hapo hakuna timu itakayoruhusiwa.
Katika hatua nyingine, Dk. Mwakyembe ameomba msaada kutoka kwa Shirikisho la Mpira Miguu Ulaya (UEFA) kupata wataalam watakaosaidia kutoa mafunzo ya kupanga ratiba ya Ligi Kuu msimu ujao.
“Haiwezekani ukawa na ligi nzuri kwa ratiba kichaa, inayokuelekeza leo uko Kagera kesho uko Mbeya, kesho kutwa uko Mwanza. Huko ni kuchosha timu na kuongeza gharama kubwa sana, kabla sijaja hapa nilikuwa na kikao na ujumbe wa watalaam kutoka UEFA.
“Nadhani tunahitaji msaada wa kitaalamu kutengeneza ratiba ya ligi kuu na daraja la kwanza, nipende kuhwahakikishia yaliyotokea hivi karibuni hayatatokea tena kwenye ligi,” ameahidi Dk. Mwakyembe.
Leave a comment