BODI ya Filamu, Baraza la Sanaa na Chama cha Hatimliki (Basata), vimeshauriwa kuungana ili vifanye kazi kwa pamoja. Anaripoti Martin Kamote…(endelea).
Ushauri huo umetolewa leo tarehe 28 Agosti 2019 na Dk. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo alipokutana na wasanii jijini Dar es Salaam.
Amesema, itapendeza kama vyombo hivyo vitashirikiana kwa pamoja ili kumuinua msanii ambaye leo hii hajanufaiki vilivyo na kazi yake.
Hata hivyo ameeleza, anasikitishwa kuwaona wasanii wanalipa pesa ili nyimbo zao zipigwe kwenye vyombo vya habari, badala ya vyombo hivyo kuwalipa wasanii kwa ajili ya kupiga nyimbo hizo.
“Watanzania tuna bahati sana, kuna majina hapa ingekuwa wapo huko Ulaya huwezi hata kumsalimia kwa mbali, lakini leo hii hakuna, sio sahihi na mimi nalisema hili kwasababu linamuuma sana mkuu wa nchi (Rais John Magufuli).
“Kuna wasanii mashuhuri lakini nashindwa kufikiria kwamba hadi leo yupo katika hali ya chini, ninahitaji ufumbuzi wa kimfumo vyombo kutokana na hilo vyote vinavyohusika na sanaa na vingine vyote viongee lugha moja,”amesema.
Aidha, Dk. Mwakyembe amesema lengo la serikali ni kuviunganisha vyombo hivyo vinavyosimamia Sanaa ili kurahisisha utendaji na kuboresha kazi ya sanaa kwa ujumla wake.
“Leo naomba nitamke mbele yenu kwamba nataka Basata, Cosota, Bodi ya Filamu na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) chini ya serikali ya awamu ya tano naomba niwashuhudie mnaongea lugha moja na vyombo vingine pia vitaongea lugha moja,” amesema.
Na kwamba, wasanii wa muziki wanapata shida kutokana na kunyanyaswa kwenye suala la muda wa kufanya kazi zao.
“Leo unapata taarifa mwanamziki mwenye heshima ya Kinkikii anapiga mziki mahali halafu mwisho saa tano usiku, huyo ameenda ofisini kwasababu yeye ofisi yake ni usiku, toka lini wewe kazi yako mwisho saa kumi ukamaliza kazi saa nane, wewe ni mchapakazi lakini huyu wa usiku akipitisha saa mbili tu shida.
“Wizi wa kazi za sanaa umegeuka kuwa haki na sasa naona unatafutiwa hata vitambulisho na unafanyika mchana kweupe hii ni kwasababu suala la sanaa katika mazingira ya sasa tuliyonayo huwezi kugusagusa hapa na pale, kunahitajika kuwe na nguvu kubwa.
Dk. Mwakyembe ameeleza kuwa bila kubadilisha sera hapatakuwa na mabadiliko
“Tumebaini wakati mchakato huu unaendelea kwamba hata hili tunaolifanya leo likifanyika bado sehemu kubwa ya changamoto zinatakiwa kushughulikiwa hivyo bila msingi wa sera kubadilika mazingira hayatabadilika”, amesema.
Ameweka wazi kuwa sera alizozikuta kwenye wizara hiyo za muda mrefu ambapo ipo sababu ya kutengeneza sera nyingi mpya.
“Mchakato umefikia mbali sana ila tukasema tuwapekekee mabingwa wa tathmini wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wiki iliyopita na tutapata muelekeo mzuri,” amesema.
Leave a comment