WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango ametangaza ‘kiaina’ kuwania Ubunge wa Buhigwe mkoani Kigoma kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Jimbo hilo kwa sasa linaongozwa na Albert Obama kupitia CCM. Obama amewaongoza wananchi wa Buhigwe tangu mwkaa 2010.
Dk. Mpango alitangaza adhima hiyo jana Alhamisi tarehe 11 Juni 2020 Bungeni jijini Dodoma, wakati akihitimisha hotuba ya Bajeti ya Serikali ya Tanzania ya mwaka 2020/21 ya Sh. 34.87 trilioni.
Katika hitimisho lake, Dk. Mpango alitoa pongezi lukuki kwa Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli jinsi alivyoliongoza Taifa hilo kwa kipindi cha miaka mine na ushehe na kuwaomba Watanzania kumchagua tena kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Dk. Mpango ambaye ni Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, alitumia fursa hiyohiyo kutangaza nia akisema, “Watanzania msisahau pia kumpatia Rais wetu wabunge na madiwani wanaomudu maadili na mwendo wa Hapa kazi Tu na kama itawapendeza wananchi wenzangu wa Buhigwe na chama chetu (CCM), basi iwe pamoja na mimi mtumishi wenu.”
Baada ya kueleza hivyo, ukumbi karibia wote wa Bunge, ulilipuka kwa shangwe za kushangilia kwa makofi na vigelegele.
Akiendelea kuhitimisha, Dk. Mpango alisema, “Nawaambia kweli Watanzania wenzangu, Rais huyu ni tunu ya thamani kubwa kwa Tanzania na utawala wake ni fursa kubwa ambayo kama hatutaitumia vizuri, basi mjue itachukua miaka mingi ijayo kuifikia Tanzania mpya tunayoitamani.
CCM internal rifts will be beneficial to the opposition camp especially Chadema!