WAKATI Chama Cha Mapinduzi (CCM), kikitarajiwa kuanza kampeni za uchaguzi wa serikali za mitaa kikiwa peke yake, Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu ameonya watakaofanya vurugu kwenye kampeni zinazotarajia kuanza tarehe 17 – 23, Novemba 2019. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Amesema, serikali imejipanga kuhakikisha mikutano ya kampeni inafanyika kwa amani na utulivu.
“Niwaase wote kwenda kwenye kampeni, serikali itasimamia kuanzia kampeni mpaka kupiga kura, kwamba itakuwa siku tulivu.
“Na niwaonye wale ambao watajitokeza kwenda kufanya fujo kwenye maeneo hayo, ambayo wananchi watakuwa wanakutana wakiwasilikiza wagombea,” ameeleza Waziri Majaliwa.
Waziri Majaliwa amewataka wananchi kushiriki katika kampeni hizo, ili kusikiliza sera za wagombea, kwa ajili ya kufanya maamuzi sahihi kwenye siku ya uchaguzi.
“Kwa hiyo tuwahakikishie usalama wa kutosha kwenye maeneo hayo. Chagua kiongozi bila ushabiki wa chama, ili upate kiongozi unayeamini atakuongoza. Wagombea wameshachukua fomu, washarudisha fomu, na keshokutwa tarehe 17 tunazindua kampeni za kuwasikiliza wanataka kutuahidi nini,” amesema Waziri Majaliwa na kuongeza;
“Natoa wito mwende mshiriki kwenye hizo kampeni, muwasilikize vizuri mkipata, nafasi ya kuwauliza maswali waulizeni, ili ujiridhishe siku utakapokuwa unampigia kura, huyu uliyeona anakufaa ndiye umpigie kura.”
Leave a comment