MKUU wa Wilaya ya Dodoma Mjini Christina Mndeme amezindua mradi wa maji katika kijiji cha Mhande huku akiwaonya watakaoharibu miundombinu ya mradi huo watachukuliwa hatua za kisheria, anaandika Mwandishi Wetu.
Mradi huo umefadhiliwa na Shirika la Wamishionari wa Damu Takatifu ya Yesu(CPPS), kutokana na maombi ya Mbunge wa Dodoma mjini, Anthony Mavunde.
Hatua hiyo ya Mavunde ilitokana na wananchi hao kukabiliwa na kero ya maji kwa muda mrefu hali iliyowalazimu kutembea zaidi ya kilomita 15 kufuata maji kijiji cha Ntyuka.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Mndeme alilishukuru shirika hilo kwa ufadhili wa mradi huo na kumpongeza Mavunde kwa kuwa mstari wa mbele kutatua kero za wanachi wake hususani maji katika kata ya Ngh’ongh’ona.
Amesema hatasita kuwachukulia hatua watu watakaoharibu miundombinu ya mradi huo wa maji kwa kuwa kumekuwepo na watu wenye nia mbaya ya kuhujumu miundombinu.
“Mwili unahitaji maji unapotafuta maji mbali roho inasononeka hata muda wa kusali unaukosa, tunashukuru sana shirika hili lakini wananchi tuna wajibu wa kuutunza mradi huu ambao ni wa thamani kubwa sana hapa tumeambiwa umegharimu kiasi cha Sh. milioni 35,” amesema
Aliwataka wananchi hao kila mmoja kuwa mlinzi wa mwenzie ili mradi huo uweze kudumu kwa muda mrefu na kuwasisitiza maji hao yatumike kwa malengo yaliyokusudiwa.
“Sasa changamoto hii ya maji imetatuliwa ninachowaomba wananchi wa Mhande mfanye kazi kwa bidii ili kujiletea maendeleo kwa kuwa awali mlipoteza muda mwingi kutafuta maji,” amesema
Leave a comment