SERIKALI ya Tanzania imesema bidhaa ya sukari imeadimika nchini, kutokana na uzalishaji wake katika msimu wa mwaka 2019/2020, kukumbwa na changamoto mbalimbali. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumanne tarehe 12 Mei 2020 na Japhet Hasunga, Waziri wa Kilimo, wakati akisoma hotuba kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya wizara hiyo, kwa mwaka wa fedha wa 2020/2021.
Hasunga ametaja changamoto hizo ni, uchakavu wa mitambo ya viwanda, kusimama kwa uzalishaji katika kipindi cha mwezi mmoja katika Kiwanda cha Sukari cha Mtibwa, kutokana na mitambo yake kuharibika.
Pamoja na uwepo wa mlipuko wa ugonjwa wa vidung’ata wa njano katika mashamba ya miwa, na mvua nyingi zinazoendelea kunyesha.
Ufafanuzi huo umekuja kipindi ambacho Tanzania inakabiliwa na uhaba mkubwa wa sukari katika baadhi ya maeneo nchini.
Katika baadhi ya maeneo sukari haipatikanani na kama inapatikana basi inauzwa hadi Sh5,000 bei ambayo ni ya juu ukilinganisha na bei elekezi iliyotangazwa isiyozidi Sh4,000 huku kwa jiji la Dar es Salaam bei elekezi ni Sh.2600.
Hasunga amesema hadi kufikia mwezi Aprili 2020, uzalishaji wa sukari ulifikia tani 298,948.61 ,sawa na asilimia 86 ya lengo la uzalishaji wa tani 345,296.
Amesema ili kukabiliana na upungufu huo, Serikali imeingiza tani 40,000 za sukari kutoka nje ya nchi, ili kufidia pengo la uzalishaji wa ndani, katika msimu wa 2019/2020.
Hasunga amesema, Serikali kupitia Bodi ya Sukari imetangaza bei elekezi ya bidhaa hiyo, ili kudhibiti mfumuko wake wa bei, unaosababishwa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu.
“Pamoja na jitihada za serikali za kuingiza sukari nchini ya kuziba pengo, kumekuwepo na changamoto ya kupanda kwa bei ya sukari kusikokuwa kwa kawaida,” amesema Hasunga na kuongeza:
“Kutokana na hali hiyo, wizara kupitia Bodi ya Sukari baada ya kufanya uchambuzi wa kina na kwa kutumia sheria ilitangaza bei elekezi ya jumla na rejareja, katika mikoa yote ya Tanzania bara kwa lengo la kukabiliana na wafanyabishara wasio waaminifu.”
Pia, Hasunga amesema Bodi ya Sukari inaendelea kuratibu uongezaji wa maeneo zaidi ya hekta 6,000, ya kilimo cha miwa kwenye maeneo ya uzalishaji wa miwa kwa ajili ya kutengeneza sukari.
Hasunga ametaja maeneo hayo kuwa ni, Hekta 2,280 inayomilikiwa na Kiwanda cha Sukari cha Bagamoyo, Hekta 2,300 zinazomilikiwa na Kiwanda cha Sukari cha Kagera, huku Kiwanda cha TPC kikimiliki Hekta 400, na Kiwanda cha Mkulazi kinamiliki hekta 1,500.
Leave a comment