NAIBU Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Juma Aweso amesema kama Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lingekuwa linatoa tuzo, angeshauri litoe kwa Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Aweso ametoa ushauri huo leo tarehe 14 Novemba 2018 bungeni jijini Dodoma mbele ya Naibu Spika Tulia Ackson, akisema kwamba Kikwete amekuwa akitetea masilahi ya wananchi wake na kwamba anastahili kupata tuzo.
“Laiti kama bunge lako lingekuwa linatoa tuzo ningeshauri litoe kwa Kikwete kutokana na kutetea wananchi wake,” amesema Aweso.
Akijibu swali la Kikwete kuhusu kusuasua kwa utekelezwaji wa mradi wa miundombinu ya maji awamu ya tatu Chalinze, Aweso amesema serikali imeamua kumrejesha kwa masharti mkandarasi wa mwanzo wa mradi huo, aliyesimamishwa kutokana na sababu mbalimbali ili aukamilishe mradi huo.
“Serikali inaendelea na uboreshaji huduma ya maji Chalinze kwa sasa serikali inatekeleza awamu ya tatu, serikali imeamua kumrejesha mkandarasi wa mwanzo ili amalize kazi, mkandarasi huyo amepewa masharti mapya ya kuhakikisha unamalizika kwa kasi, anatakiwa kukamilisha Desemba 2018 wizara itaendelea kufuatilia akamilishe kazi, na asipofanya hivyo atachukuliwa hatua,” amesema Aweso.
Leave a comment