TAKRIBANI watu 60 wanaohofiwa kufariki dunia huku wengine mamia wakiungua moto baada ya lori la mafuta kupinduka na baadaye kuwaka moto, katika eneo la Msamvu, mkoani Morogoro. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa kutoka eneo la tukio zinasema, lori hilo ambalo lilikuwa limebeba mafuta ya petroli, liliwaka moto muda mfupi baada ya kupinduka.
Mmoja wa mashuhuda wa ajali hiyo ameliambia MwanaHALISI ONLINE, aliyejitambulisha kwa jina moja la Petro, ameeleza kwamba vifo vya watu hao pamoja na majeruhi wake, vimesababishwa na wao kuanza kuchota mafuta yaliyokuwamo kwenye gari hilo.
“Gari hili lilikuwa limebeba mafuta. Limepinduka muda mfupi baada ya kupata ajali,” ameeleza Petro na kuongeza, “wengi wa wahanga wa tukio hili, ni wale ambao walivamia gari hilo na kuanza kuchota mafuta.”
Petro amesema, “binafsi nimeanguka katika ile msukumeni, baada ya kufanikiwa kutoka kule nimekuta watu wanagombania mafuta kama maji, watu wako bize hawalewi kwamba haya mafuta au maji au nini, wako bize na lori limelipuka pale pale na watu kuanza kutafutana.”
Tukio hili la kusikitisha limetokea leo Jumamosi 10 Agosti 2019, ambapo MwanaHALISI ONLINE limefika eneo hilo la tukio na kushuhudia miili iliyoungua ikiwa imelazwa pembeni ya barabara ya Dar es Salaam – Morogoro.
Kwa mujibu wa wenyeji wa eneo hili, wengi wa waliofariki dunia ama kujeruhiwa kwa kuungua kwa moto, ni madereva bodaboda na mamalishe wanaofanya shughuli zao mahali hapo.
“Gari imepata ajali watu wakaanza kuchota mafuta. Katokea mjuaji mmoja kakimbilia kuiba betri ya gari, ndipo shoti ilipotokea likaripuka na kuunguza wenye madumu, pikipiki na waliokuwa karibu,” ameeleza mmoja wa mashuhuda.
Kamanda wa Polisi mkoani Morogoro, Wilbroad Mutafungwa amesema, karibu watu 57 wamepoteza maisha katika ajali hiyo iliyotokea saa mbili asubuhi. Anasema, ajali hiyo imetokea umbali wa mita takribani 200 kutoka kituo kikuu cha mabasi Msamvu ukitokea Dar es Salaam.
Leave a comment