SERIKALI ya Tanzania imetahadharisha wananchi wake, juu ya hatari ya ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwa na mlipuko wa Virusi vya Corona, unaotikisa dunia hivi sasa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 29 Februari 2020, Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, amewataka Watanzania kuepuka vitendo vinavyoweza pelekea maambukizi ya ugonjwa huo.
Waziri Ummy amewataka Watanzania, kukwepa, kupeana mikono, kukumbatiana na kupigana mabusu, katika kipindi hiki ambacho mlipuko huo umeshika kasi.
“Katika kipindi hiki ambacho kuna tishio la ugonjwa wa Corona, ninawataka wananchi kujizuia kupeana mikono, kukumbatiana na kubusiana hili linaweza kuwa gumu kwa Watanzania ila lazima niliseme,” amesema Waziri Ummy.
Wakati huo huo, Waziri Ummy ametoa siku tatu kwa kila Mkoa nchini, kuwasilisha jina la kituo maalumu, kilichotengwa kwa ajili ya kuhudumia washukiwa au wagonjwa wa Covid-19.
Hadi sasa virusi hivyo vimesambaa zaidi ya nchi 50 duniani, na kuuwa maelfu ya watu. Huku nchi ya China ikiwa mhanga mkubwa wa ugonjwa huo.
Hata hivyo, Waziri Ummy amesema Tanzania haina mgonjwa wa Covid-19.
Leave a comment