MWILI wa Benjamin Mkapa, Hayati Rais Mstaafu wa awamu ya tatu ya Tanzania, unaendelea kutolewa heshima za mwisho na Watanzania, katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Mwili wa Mkapa umefikishwa katika uwanja huo saa 2 asubuhi leo Jumatatu tarehe 27 Julai 2020 ikiwa ni siku ya pili kati ya tatu za kuuaga kabla ya kupelekwa kijijini kwake kwa maziko yatakayofanyika Jumatano tarehe 29 Julai 2020.
Soma zaidi:-
Mawaziri na manaibu waziri pamoja na makatibu wakuu wa serikali zote wamefika viwanjani hapo kwa ajili ya kuuaga mwili wake.
Pia, wakuu wa mikoa na wilaya pamoja na viongozi wa taasisi za umma wataungana na Watanzania kutoa heshima zao za mwisho kwa mwili wa Mkapa.
Mkapa aliyezaliwa tarehe 12 Novemba 1938 alifariki dunia Alhamisi tarehe 23 Julai 2020 hospitalini jijini Dar es Salaam kwa mshituko wa moyo.
Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ameongoza zoezi hilo, ambapo aliwakaribisha Watanzania kuanza kuuaga mwili huo.
“Tunatambua uwepo wenu Watanzania wote kwa kuendelea kushirikiana na serikali katika jambo hili kubwa la kitaifa.”
“Leo tunaendelea na siku ya pili ya maombolezo na kuaga mwili wa baba yetu mpendwa Rais mstaafu Mkapa, nawakaribisheni wote, tunatambua uwepo wenu ambao mpo uwanja huu wa Uhuru,” amesema Mhagama.
Mhagama amesema, shughuli ya kuuaga mwili wa Mkapa itafanyika mpaka usiku na hatimaye kumalizika kesho kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari mbalimbali
Leave a comment