WATANZANIA 64 wamehukumiwa kulipa faini zaidi ya Sh.25 million au kwenda jela mwaka mmoja kwa kosa la kwenda nje ya nchi bila kibali. Anaripoti Brightness Boaz, Dar es Salaam … (endelea).
Hukumu hiyo ilitolewa jana Jumatatu tarehe 25 Januari 2021, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, baada ya washtakiwa hao, kukiri kosa lao mbele ya mahakimu wawili tofauti, Huruma Shaidi na Agustino Mbando.
Wakili wa Serikali, Shija Sitta alisema, tarehe 22 January 2021, washtakiwa hao walikamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, wakiwasili kutoka nje ya nchi katika tarehe zisizo julikana kwenda Afrika ya Kusini bila kufuata taratibu.
Sitta na wakili mwezake wa Serikali, Godfrey Ngwijo alisema baada ya kukamatwa kwa washtakiwa hao, walipelekwa ofisi za uhamiaji zilizopo Kurasini jijini Dar es Salama ambapo walichukuliwa maelezo ya awali kabla ya kufikishwa mahakamani kujibu shtaka lililokuwa mbele yao.
Hata hivyo, mawakili hao walisema, washtakiwa walikiri kutenda kosa hilo na kuisababishia Serikali hasara iliyotokana na gharama za kuwarejesha nchini Tanzania na kuiomba Mahakama kuwapa adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine.
Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi aliwahukumu washtakiwa 32 kati ya 64, kulipa faini ya Sh.500,000 kila mmoja au kwenda jela mwaka mmoja.
Baadhi ya washtakiwa hao, walikidhi vigezo vya kwa kulipa faini hiyo huku wengine wakipelekwa gerezani kwa kushindwa kutimiza masharti.
Leave a comment