CHAMA cha Wafamasia nchini (PST), kimeiomba serikali kusaidiana nacho ili kuhakikisha wanatokomeza tatizo la usugu wa dawa za binadamu, anaandika Mwandishi wetu.
PST kimesema tatizo hilo husababisha vifo na kwamba wakishirikiana na serikali wanaweza kuliondoa.
Hayo yameelezwa na Katibu mkuu wa chama hicho, Geofrey Yambayamba katika shule ya wasichana Msalato iliyopo Dodoma wakati wa kuhitimisha kampeni ya mwezi mmoja ya kutoa elimu ya madhara yanayotokana na usugu wa dawa.
Amesema kundi linalokabiliwa na tatizo la usugu wa dawa ni pamoja na wanafunzi wa sekondari kwa kuwa hawamalizi dozi wanapoandikiwa na daktari.
“Wanafunzi wengi wa shule za sekondari ni miongoni mwa watu waliopo hatarini kupatwa na usugu wa dawa kutokana na ukweli kwamba mara nyingi huwa hawamalizi dozi na kusababisha magonjwa kujirudia rudia”alisema.
Amewataka wanafunzi hao kufikisha elimu kwa jamii kuhusu matumizi sahihi ya dawa na kwamba kila mtu anatakiwa kutumia dawa ambazo hazijaisha muda wake.
Leave a comment