WASTAAFU wametakiwa kubuni miradi ambayo itawawezesha kufanya shughuli ya ujasiriamali kwa lengo la kujiongezea kipato baada ya kustaafu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yameelezwa na Mshauri mwelekezi na Mratibu wa Mafunzo mafupi na ushauri wa Kitaalam Dk.Hassanal Isaya katika mafunzo ya ujasiriamali kwa wastaafu watarajiwa katika mwaka wa fedha 2020/21 kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia yaliyofanyika Jijini Dodoma.
Katika mafunzo hayo ya siku tano kwa wastaafu watarajiwa 150 kutoka Wizara hiyo yalifunguliwa juzi na Mwenyekiti wa kamati ya Mafunzo ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa niaba ya Katibu mkuu Wizara ya Elimu, Prof. James Mdoe.
Akitoa elimu ya Ujasiriamali mwezeshaji huyo alisema kuwa baada ya kustaafu ni vyema kuangalia mazingira rafiki ya kufanya ujasiriamali kuwa na mipango ambayo haiwezi kumsababishia hasara.
Aidha alisema kuwa ili kuweza kufanya vizuri katika ujasiriamali ni lazima kufanya kazi kwa bidii sambamba na kuwa mbunifu katika kufanya shughuli ya kumwingizia kipato.
“Ili uwe mjasiriamali mzuri ni lazima uweze kufanya kazi kwa bidii na kuwa mbunifu katika kuibua miradi na kuboresha bidhaa ambazo unazipeleka sokoni.
“Tunajua wakati wa utumishi mlikuwa mkifanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu lakini katika ujasiriamali hakuna sheria za aina hiyo hivyo ni wewe mwenyewe unayeweza kufanya kazi kwa muda ulioupanga,” alisema Dk. Isaya.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti washiriki hao katika Mafunzo ya kujiandaa kustaafu kwa Watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknologia wanaotarajia kustaafu utumishi wa Umma, walisema kuwa mafunzo hayo yameweza kuwasaidia kuelewa mambo mengi ambayo walikuwa hawayajui.
Mmoja wa washiriki Remidius Kisanko ambaye ni mkufunzi kutoka chuo cha ualimu Sumbawanga alisema kuwa mafunzo hayo yamewafanya kuelewa nini wanachotakiwa kukifanya baada ya kustaafu.
“Tumeweza kujifunza mambo ya kijiepusha nayo wakati wa kustaafu,pia tumeweza kujua nini kinaweza kusababisha msongo wa mawazo kwa wataafu.
“Tumefundishwa jinsi ya kuepukana na msongo wa Mawazo pindi tunapokuwa tumestaafu,lakini pamoja na hayo tunaiomba Wizara kuona uwezekano wa kutoa mafunzo mapema kwa wale ambao bado hawajafikia hatua ya kustaafu,” alisema Kisanko.
Naye Hadija Madaha kutoka Wizara ya Elimu Makao makuu alisema amepata faraja sana kupitia mafunzo hayo hususani katika kipengele cha upandishwaji wa Madaraja.
Alisema kuwa yeye alianza kazi mwaka 1974 lakini alipandishwa daraja mara moja tu jambo ambalo alisema lilionekana kumuumiza hasa wakati huo ambao anatarajia kustaafu.
Akizungumzia ujasiriamali alisema kuwa amejifunza ni namna gani ya kuweza kuendesha miradi baada ya kustaafu badala ya kujiingiza katika mikopo mbalimbali.
Leave a comment