SERIKALI imetakiwa kuhakikisha waraka wa mishahara unapitiwa kila baada ya miaka mitatu na kufanyiwa marekebisho kama inavyotakiwa kisheria ili kuhakikisha haki ya ujira stahiki na kuishi katika hali inayofaa zinazingatiwa. Anaripoti Regina Kelvin…(endelea).
Wito huo umetolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) kupitia mapendekezo yaliyowekwa katika Ripoti ya Haki za Binadamu na Biashara ya mwaka 2017 iliyozinduliwa jana tarehe 16 Agosti, 2018.
“Serikali ihakikishe waraka wa serikali kuhusu Mishahara unapitiwa kila baada ya miaka mitatu kama inavyotakiwa kisheria na kufanyiwa marekebisho ili kuhakikisha haki ya ujira stahiki na haki ya kuishi katika hali inayofaa zinazingatiwa,” imependekeza LHRC kupitia ripoti hiyo.
Mapendekezo hayo yamefuatia baada ya matokeo ya utafiti wa ripoti hiyo kubaini kwamba, waraka wa serikali kuhusu viwango vya mishahara unaotumika ni wa mwaka 2013 na kwamba viwango hivyo havitoshelezi ukizingatia gharama za maisha ambazo zinapanda kila mwaka.
“Malalamiko ya mishahara duni yaliyotolewa na wafanyakazi katika mikoa 15 iliyotembelewa, maofisa kutoka vyama vya wafanyakazi walisema kwamba viwango vya chini vya mishahara kwenye waraka wa serikali wa mwaka 2018 havitoshelezi.
“Baadhi ya wafanyakazi waliohojiwa walilalamika kwamba wakiomba kuongezewa mishahara wanatishiwa kufukuzwa au kuambiwa kuacha kazi,” imeeleza sehemu ya ripoti hiyo.
Leave a comment