WANAWAKE wanaofanya biashara ya kuuza samaki maeneo ya stendi kuu ya mabasi mjini hapa wameilalamikia Halmashauri ya Mji wa Babati kuwaondoa kwa nguvu na kuwasweka rumande bila kuwaandalia mazingira mengine, anaandika Mwandishi Wetu.
Malalamiko hayo waliyatoa wakati wakizungumza na wakiwa maeneo ya zima moto ilipo ofisi ya kata walipokuwa wameswekwa rumande ya kata kabla ya kuwafikisha kituo cha polisi cha Babati.
“Sisi tuna uwezo mdogo wa kifedha na mitaji yetu haizidi Sh 20,000 wakituondoa hapa tutaenda wapi maana kule wanakolazimisha tuende hamna wateja kwa kua sisi tunawauzia wasafiri,’’alisema Janeth Edison.
Wachuuzi hao walisema wanashindwa kukubaliana na matakwa ya Halmashauri kwa kuwa eneo wanaloambiwa kupewa sokoni ni nyuma sana ambako hawawezi kupata wateja.
Aidha, wanasema baadhi ya watumishi wa Halmashauri wamewageuza kitega uchumi chao kwa kua wanawatoza faini ya Sh 90,000 lakini wakati wakiandika risiti wanaandika wamelipia 50000 suala ambalo walidai linawaumiza.
“Tulipoenda kwa Kaimu Mkurugenzi, Bashir Mhoja, alituambia hawatatutafutia eneo jingine tulipomfuata ofisini badala yake alisema watatukamata na kututoza faini au kutufikisha mahakamani,’’ alisema Zakia Amani.
Naye Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Babati Mjini, Fauswali Hamadi, alisema ni vizuri tatizo hilo likamalizwa kwa busara.
Alisema Rais John Magufuli alishatangaza mara kwa mara kwamba wafanyabiashara ndogondogo (wamachinga) waachwe wakiendelea na bishashara zao.
Leave a comment