WANAUME wanaopewa likizo ya uzazi, wameshauriwa kutumia vizuri kwa kumsaidia mama aliyejifungua, na kwamba ni kwa mujibu wa sheria ya kazi na ajira ya mwaka 2004. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa jijini Dodoma leo tarehe 2 Agosti 2019 na Ummy Mwalimu, Waziri wa afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto mbele ya vyombo vya habari kuhusu maashimisho ya wiki ya unyonyeshaji duniani.
Akitoa tamko la serikali kuhusu kuanza kwa wiki ya unyonyeshaji Waziri Mwalimu amesema, likizo ya wanaume sio kwa ajili ya kwenda kustarehe kwenye Bar, bali ni kwa ajili ya kutoa usaidizi kisaikolojia kwa wanawake waliojifungua.
“Tunapokea malalamiko kwamba baadhi ya wanaume wanaopewa likizo ya uzazi, huwa hawaonekani kabisa nyumbani na wengine hutumia siku hizo tano kwa ajili ya kustarehe na wanawake wengine, hii haiko sawa kisheria,” amesema.
Mbali na hayo amesema, kimsingi likizo hiyo ni maalumu kwa ajili ya baba kumsaidia mama majukumu ya kifamilia anapokuwa amejifungua, na si vinginevyo.
“Wizara yetu itafanya utafiti kama kweli likizo hii ina manufaa, na kama tukijiridhisha kuwa haina manufaa lazima tuifute,” amesisitiza.
Pamoja na hayo amewataka waajiri kuzingatia sheria ya ajira na mahusiano kazini, kwa kumpatia haki ya kunyonyesha mama aliyejifungua.
“Wanawake wanaonyimwa haki hii, watoe taarifa kwa maofisa kazi katika halmashauri zao kwasababu msipojitokeza kudai haki yenu, sisi hayutaweza kujua,” amesisitiza.
Leave a comment