WATU watatu wanashikiliwa na jeshi la polisi mkoani hapa kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo la dawa ya kuleya aina ya bangi, anaandika Christina Haule.
Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Leonce Rwegasira tukio la kwanza lilitokea Septemba 26 saa 9 usiku katika eneo la Mikese mizani kata na tarafa ya Mikese wilayani Morogoro Vijijini.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Iddi Juma (42) dereva na mkazi wa Tabata Segerea jijini Dar es salaam na Aniset Ferdinand (30) mkazi wa Tabata Chang’ombe.
Kamanda Rwegasira amesema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa na kupekuliwa na askari polisi waliokuwa doria na kukutwa na bangi viroba 6 inayokadiriwa kuwa na uzito wa kilo 80 wakiisafirisha kwenda Dar es salaam ikiwa kwenye gari lenye namba za usajili T438 ARN aina ya Toyota Corsa.
Amesema, watuhumiwa pamoja na gari wanashikiliwa na polisi kituo cha Mikese huku hatua za kuwafikisha mahakamani zikiendelea.
Katika tukio jingine Ally Daudi anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kukamatwa na vichane 27 vya Mirungi akiwa amevihifadhi kwenye mfuko wa sandarusi wa rangi ya bluu.
Kamanda Rwegasira amesema, mtuhumiwa huyo alikamatwa na askari waliokuwa doria septemba 27 saa 10 jioni katika maeneo ya Vibandani Manispaa ya Morogoro na kwamba anatarajia kufikishwa mahamani.
Leave a comment