RAIS John Magufuli amewataka watu wanaolalamika bei ya mahindi kupanda, wakalime ya kwao, ili yawe ya bei ya chini. Anaripoti Regina Mkonde … (endela).
Mkuu huyo wa nchi ametoa kauli hiyo leo tarehe 20 Novemba 2019, wakati akizungumza na wananchi mkoani Morogoro.
“Ukiona wengine wachache wanalalamika bei ya mahindi iko juu, na nataka wakulima washangilie zaidi. Tulizungumze hili wazi, kwa Watanzania wote, ukiona mahindi yako juu, nenda kalime yako ya bei ya chini, biashara hii lazima iwe huru,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli amesema katika uongozi wake, hatawapangia bei wakulima, kwa kuwa anafahamu shida wanazopitia wakati wa kulima na hata kuvuna mazao yao.
“Katika kipindi changu sitapanga bei ya mkulima, na mimi ni mtoto wa mkulima ninafahamu maana ya kulima, sasa wale wanaotaka bei nzuri ya mazao, huu ndio wakati kutengenza bei nzuri, mvua zimeanza kunyesha na wewe ukawe na kashamba kako,” amesema Rais Magufuli na kuongeza;
“Mkulima anatafuta mbolea, anahangaika kule anafukuzana na nyoka matope ni yake,wakati wa kuvuna ni yeye,halafu avune umpangie bei..bei itajipanga yenyewe,wakati wa kuwapangia bei wakulima mazao yao umeshakwisha.”
Kauli hiyo ya Rais Magufuli imekuja kukiwa na malalamiko ya bei ya baadhi ya bidhaa kupanda, ikiwemo unga wa mahindi.
Hivi karibuni Dk. Ashatu Kijaji, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango akiwa bungeni jijini Dodoma, alisema bei ya bidhaa za chakula ikiwemo unga wa mahindi, imepanda kutokana na baadhi ya maeneo hayakupata chakula cha kutosha.
Leave a comment