MKUU wa Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa, Jamhuri William ametoa wito kwa wadau waliopo mkoani humo na halmashauri ya wilaya ya Mufindi kuendelea kushirikiana katika miradi ya maji, afya na usafi wa mazingira. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Ameyaeleza hayo katika maadhimisho ya wiki ya Usafi wa Mazingira kwa halmashauri ya wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa yaliyofanyika jana katika kijji cha Kitelewasi kilichopo Kata ya Mbalamaziwa.
Jamhuri amewaomba shirika la Maendeleo ya Watu (PDF) na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Watoto (UNICEF) kuendelea kushiriki katika kampeni ya kuweka wilaya ya Mufindi katika hali ya usafi.
Akitoa shukrani mwakilishi wa UNICEF, Remigius Sungu alisema wanatambua changamoto zilizopo katika program za WASH na itaendelea kushirikiana na Halmashauri kutokana na ufanisi na ubora wa kazi zinazoendelea ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vyoo bora kwa shule za Msingi na vituo vya kutolea huduma za Afya.
Wakifafanua miradi inayoendelea mwakilishi wa PDF Mufindi, Injinia Elias Erasmus na Johaness Rumito wamesema wamepata ushirikiano mkubwa toka kwa uongozi wa halmashauri katika utekelezaji wa miradi inayoendelea ya ujenzi wa vyoo bora kwa shule tano za msingi katika halmashauri ya wilaya ya Mufindi za Malangali, Mpeme, Mninga B, Sadani na Lugodalutali, vituo vya kutolea huduma za afya vya Kasanga na Dispensari ya Igombavanu.
Maadhmisho hayo yanayofanyika kila mwaka Tanzania ambayo ni sehemu ya kampeni ya taifa ya usafi wa mazingira na malengo ya milenia (lengo namba 7C-Afya na Usafi wa mzingira) yalihitimishwa kwa shirika la PDF kugawa masinki ya Plastic yajulikanayo kama SATO na kutoa elimu ya namna ya kutibu maji ya kunywa kwa kutumia vidonge vya AQUA TABS ambayo ni njia rahisi ya kuokoa muda na rasilimali kuni kwa kuchemsha maji.
Leave a comment