BAADHI ya wakazi wa kata ya Mkata, Handeni, mkoani Tanga, wamesema kuwa kitendo cha serikali kuwapelekea mradi wa maji safi kimewafanya kuondokana na kupata maji kwa taabu. Anaripoti Danson Kaijage, Handeni … (endelea).
Mbali na kupata maji kwa taabu wameeleza kuwa kabla ya kupokea Mradi wa maji wa kata ya Mkata walikuwa wakitumia muda mwingi kufuata maji mbali huku hali ya uzalishaji ikidorora kutokana na kutumia muda mwingi kutafuta maji tena kwa foleni.
Wakazi hao waliokuwa wananunua dumu la maji la lita 20 kwa Tsh.500 mpaka Tsh.1,000 hivi sasa wananunua kwa Tsh. 50.
Baadhi ya kina mama waliokutwa wakichota maji katika vituo malum vilivyojengwa na serikali, wamesema kuletewa mradi wa maji katika maeneo yao ni sawa na kukombolewa katika utumwa wa kuhangaikia maji.
“Tulikuwa tunanunua maji kwa gharama kubwa na wakati mwingine yalikuwa hayapatikani hata ukiwa na pesa mkononi, tulilazimika kutumia masaa mawili mpaka matatu kushuka mabondeni kufuata maji, tena yenye chumvi yasiyoweza kunyweka ambayo tukinunua ndoo moja kwa Tsh.100,” anaeleza Aziza Mwinjuma.
Aziza anawaomba wahusika wanaoshughulikia mradi huo kuongeza siku za kufungulia maji, ambapo anasema kwa sasa maji yanatoka siku mbili kwa wiki.
Hata hivyo, bado wananchi wa Mkata wanaona vituo vilivyowekwa kuchotea maji havitoshi, hivyo wanaiomba serikali waongeze.
“Kwanza niishukuru serikali kwa kutukumbuka kutokana na adhabu tuliyokuwa tunaipata, lakini niwaombe wahusika watuongezee mabomba, hapa tuna bomba moja ambalo halitoshi, tuko watu wengi kiasi kwamba wakati mwingine mpaka unatokea ugomvi kugombania maji,” anasema Sakina Mbega.
Mradi wa maji wa Mkata ni mradi wa serikali uliyojengwa kupitia kampuni ya Tansino Logistic Limited.
Leave a comment