WANAFUNZI wa wanaopata ujauzito kutorudi shuleni wamezidi kumkera Rais John Magufuli kwani pamoja na kupiga marufuku, amekuwa akiendelea kuchimba ‘mkwara’ kila anapopata nafasi, anaandika Irene Emmanuel.
Rais Magufuli alishapiga marufuku wanafunzi wanaopata ujauzito kurudi shuleni na kuzuia asasi zisizo za kiserikali kuendelea kutetea hilo, lakini pamoja hayo bado amezidi kupinga kila anapopata nafasi ya kufanya hivyo.
Akiwa katika uzinduzi wa nyumba za wahudumu wa afya wilayani Chato, Rais Magufuli amerudia tena katazo hilo na kuzitaka taasisi zinazounga mkono hoja za kutetea wanafunzi wanaopata ujauzito kufanya kazi za maendeleo ya jamii.
Amesema kuwa hoja hiyo inakosesha heshima Taifa kwa kujenga picha ya ubakaji, kwamba si kila aliepata mimba amebakwa, wengine wanajitakia na kuruhusu hilo itapelekea wimbi la wajawazito mashuleni.
“Ati kila aliepata mimba amebakwa? Hata kwenye familia yangu wapo waliopata mimba, wala hawakubakwa. Wasije watu wakaharibu heshima na tamaduni za kitanzania zilizojengeka muda mrefu” Alihoji Rais Magufuli.
Rais Magufuli ameziomba taasisi zingine ziige mfano wa taasisi ya Mkapa Foundation kufanya mambo ya maendeleo na wasiishie kupiga kelele majukwaani, taasisi ya Mkapa imejenga nyumba 450 huku zikiwa zimebaki nyumba thelathini.
Ameendelea kwa kuitaka serikali kusaidia kifedha taasisi kama ya Mkapa Foundation zinazojali maendeleo na kuzinyima fedha taasisi zile zinazounga mkono watoto kupata mimba na kuzaa wakiwa shuleni.
Leave a comment