WANAFUNZI wa Shule ya Msingi Ndola, iliyopo kata ya Nsalala, Mbalizi, mkoani Mbeya, wanalazimika kukaa chini ya miti kujisomea kutokana na upungufu wa vyumba vya madarasa shule hapo, anaandika Esther Macha.
Hayo yamesemwa mwishoni mwa wiki na Diwani wa Kata ya Nsalala, Crisman Mwangomale wakati wa mkutano na wananchi wake, ambapo alieleza kuwa wanafunzi wa awali na wengine hulazimika kukaa chini ya mti na kipindi cha masika hushindwa kuhudhuria masomo kwa sababu ya kukosa sehemu ya kujisomea.
Diwani Mwangomale amesema kwa sasa kila chumba kimoja cha darasa kinabeba wanafunzi 170 jambo ambalo alidai linapunguza umakini wa kusikiliza masomo na hata mwalimu kupata changamoto ya kufundisha.
“Hali ya Shule yetu ni mbaya, juzi nilipita shule hapo nikawakuta watoto wetu wamekaa chini ya mti wanajisomea, nafahamu changamoto hiyo na nimewasiliana na wenyeviti wa vitongoji ili kuitatua changamoto hiyo,” amesema Mwangomale.
Aidha Mwangomale amesema vitongoji vitatu ambavyo ni Ndola, Msikamano na Tunduma Road ndio vyenye dhamana ya kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa.
Amesema mara baada ya kukaa na viongozi wa vitongoji hivyo walipata idadi ya wananchi ambao ni nguvu kazi takribani 3,543 ambao watachangia ujenzi wa vyumba vinne vya madarasa na kutokana na hali ngumu ya maisha wamekubaliana kuanza ujenzi wa vyumba viwili, ambapo kila mwananchi atachangia Sh. 5,000.
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, ambaye pia ni kaimu Afisa Elimu wa Kata, Lucia Thamba, amesema idadi kubwa ya wanafunzi shuleni hapo imesababisha kuwepo kwa changamoto hiyo, ambapo alidai mpaka sasa shule hiyo inajumla ya wanafunzi 1,425, huku idadi ya vyumba vilivyopo ikiwa ni nane na mahitaji ikiwa ni 28.
Thamba amesema kupitia mchango wa Diwani wa Kata anaimani changamoto ya uhaba wa vyumba vya madarasa lakini pia ujenzi wa matundu 16 ya vyoo shuleni utakamilika mara baada ya mpya.
“Napongeza jitihada za Diwani, ametusaidia kubeba changamoto hizi shuleni hapa, miaka miwili ya uongozi wake amekuwa mstari wa mbele kushughulikia masuala ya elimu,” amesema Thamba.
Thamba aliwataka wananchi kujitoa katika mchango huo, na kuitaka jamii kutoitegemea serikali kuanza ujenzi huo na badala yake itaweka nguvu endapo wananchi wataonyesha jitihada.
Mmoja wa wananchi, Emmanuel Mwakalobo, alisema yuko tayari kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa na kuwataka wananchi kuungana ili watoto wasome kwenye mazingira mazuri.
Leave a comment