KAMATI ya Maadili ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imemfungia maisha kutojiusisha na soka Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho hilo, Michael Wambura baada ya kukutwa na hatia katika mashitaka matatu yaliyokuwa yakimkabili. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Wambura amekupewa adhabu hiyo baada ya kukutwa na hatia ya kupokea fedha zisizo halali kiasi cha Sh. 84 milioni, pamoja na kukutwa na hatia ya kujipatia fedha, kwa njia ya udanganyifu na kughushi nyaraka sambamba na kula njama ya kulipwa fedha na waliokuwa viongozi wa TFF Jamari Malinzi na Celestine Mwesigwa ambao kwa sasa wanakabiliwa na kesi Mahakamani.
Kamati hiyo imetoa hukumu kwa Wambura kutojihusisha na soka kwa mujibu wa kifungu cha 73(1) (c) cha Kanuni za Maadili ya TFF Toleo la 2013. Baada ya kupatikana na makosa matatu, kamati hiyo ya maadili imefika maamuzi hayo kwenye kikao chao walichokutana jana (Jumatano).
Jana mchana afisa habari wa TFF Clifford Mario Ndimbo aliwaambia waandishi wa habari kwamba Wambura amefanya makosa hayo huku akijua anashusha hadhi ya shirikisho hilo ikiwa ni kinyume na katiba ya TFF.
Leave a comment