MAMA Samia Suluhu Hassan, Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ameagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) iwashughulikie watu waliodhurumu fedha za malipo ya korosho kupitia Chama cha Ushirika cha Msingi cha Mazao(AMCOS). Anaripoti Mwandishi Wetu, Mtwara … (endelea).
Samia ametoa agizo hilo leo Alhamisi tarehe 10 Septemba 2020 wakati akihutubia mkutano wa kampeni za CCM katika Uwanja wa Polisi Jimbo la Nanyamba mkoani Nanyamba mkoani Mtwara.
Samia ameiagiza Takukuru ihakikishe waliodhurumiwa fedha za korosho walipwe stahiki zao.
“Kulikuwa na deni kubwa la korosho na Serikali tumelipa lote, lakini viongozi wa AMCOS wameangalia nani hajui kusoma pesa zao wakazichukua, naiagiza Serikali ya Mkoa kila aliyedhurumiwa kupitia Takukuru pesa ipatikane,” amesema Samia.
Amesema Serikali inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli imelipa deni lote la fedha za korosho, hivyo wanaolalamika hawajapata fedha mamlaka husika zinatakiwa zitafute ufumbuzi wa mahali ziliko fedha zao.
“Serikali tumelipa deni lote, lakini viongozi wa ushirika wanafanya mambo yasiyoingilika akilini, Rais Magufuli alishatoa Sh.20 bilioni kwa malipo ya Korosho, zipo Mtwara zitafutwe wapi zimeingia wanaodai walipwe pesa zao,” amesema Samia.
Mgombea huyo wa urais amemaliza mkutano wake wa kwanza kati ya miwili na sasa ameondoka kwenda kuendelea na mkutano mwingine mkoani humo.
Leave a comment