UPO upungufu wa walimu 24,716 wa masomo ya Sayansi na Hisabati nchini, ametangaza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknologia, Stella Manyanya, wakati akijibu swali la mbunge wa Viti Maalum, Suzan Lyimo (Chadema), anaandika Dany Tibason.
Katika swali lake, mbunge huyo alitaka kujua Waziri alipata wapi mamlaka ya kutangaza kuwa vijana wote wa elimu ya msingi hadi kidato cha nne wasome masomo yote ya sayansi.
Pia alitaka kufahamu kama kulifanywa utafiti ulioleta majibu ya kuhalalisha vijana wote kusoma sayansi yaani Kemia na Fizikia.
Naibu Waziri Manyanya amesema sehemu ya pili ya kipengele cha 11 kipengele Na.4(1) na Na 5(f) cha Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 1995, inampa mamlaka waziri kutangaza jambo lolote lenye maslahi kwa taifa kutokana na hali halisi iliyopo kwa wakati huo.
Amesema imeonekana haja kubwa ya kuhamasisha ongezeko la wanasayansi kwa kuwa wanahitajika na kwamba upungufu huo ndio uthibitisho wa muono huo.
Naibu waziri Manyanya amesema ukiacha upungufu wa walimu 24,716 wa Sayansi na Hisabati, upo upungufu wa walimu 355 wa masomo ya ufundi kwa shule za sekondari za ufundi na upungufu wa mafundi sanifu takribani 10,000 wa maabara za shule.
Amesema wizara haijawahi kutoa waraka wowote unaowataka wanafunzi wote kusoma masomo ya sayansi; badala yake imejikita katika kuimarisha miundombinu ya maabara, vifaa vya kufundishia na kujifunzia na kupeleka walimu wa sayansi shuleni.
Mbunge Lyimo katika maelezo yaliyotangulia swali lake, amesema, “Sera ya Elimu ya mwaka 2014 inaeleza wazi kuhusu mitaala na utaratibu wa masomo katika elimu ya msingi (Kidato cha 1-4) na inasema watoto wa kidato cha 1-4 watasoma masomo yote ya sayansi na wanapoingia katika kidato cha tatu watachagua masomo wanayoyataka kutokana na uwezo wao.
“Je Waziri alipata wapi mamlaka ya kutangaza kuwa vijana wote wa elimu ya msingi hadi kidato cha nne kusoma masomo yote ya sayansi.”
Leave a comment