WALIMU watatu wa Shule ya Sekondari y aKutwa Kalenge (Kalenge Day), Biharamulo, Kagera wanashikiliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwa madai ya kugawa namba ya mwanafunzi waliyemfukuza kwa mwanafunzi mwingine katika Mtihani wa Kidato cha Nne wa mwaka 2019. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu tarehe 6 Julai 2020 na John Joseph, Mkuu wa Takukuru mkoani Kagera.
Walimu wanaoshikiliwa ni Boniphace Eliab, mkuu wa shule hiyo; Edwin Valentine, makamu mkuu wa shule hiyo na Gervas Richard, Mwalimu wa Taaluma.
“Tunawashikilia waalimu watatu kwa tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi chini ya kifungu cha 31 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa namba 11/2007, kwa kufanya usajili kwa udanganyifu chini ya kifungu cha 309 cha Sheria ya Kanuni za Adhabu Sura ya 16 (Kama ilivyorekebishwa mwaka 2002),” amesema Joseph.
Joseph amesema, watuhumiwa hao walifanya udanganyifu kwa kutumia njia za rushwa, kutoa namba ya mtihani ya mwanafunzi waliyemfukuza shule, kwa mwanafunzi mwingine.
“Uchunguzi wa ulibaini walimu hawa walimfukuza shule mwanafunzi mmoja ambaye jina lake limehifadhiwa kwa kisingizo cha kuwa mgonjwa, mitihani ulipofika, kwa njia za rushwa waliitumia namba ya mwanafunzi huyo aliyefukuzwa kumpatia mwanafunzi mwingine ambaye aliufanya mtihani huo,” amesema Joseph.
Mkuu huyo wa Takukuru Kagera amesema, udanganyifu huo ulibaika baada ya mzazi wa mwanafunzi ambaye hakufanya mtihani huo, kuona jina la mwanaye kwenye matokeo.
“Uchunguzi wetu umebaini pia kuwa, mara baada ya matokeo ya kidato cha nne kutoka, jina la mwanafunzi aliyekuwa amefukuzwa lilionekana kuwa amefaulu kwa kupata daraja la pili (Division two). huku ikifahamika kuwa mwanafunzi halisi mwenye jina hilo alishafukuzwa na hakufanya mitihani,” amesema Joseph na kuongeza:
“Hali hii ilimfanya mzazi wa mwanafunzi aliyekuwa amefukuzwa shule kushikwa na mshangao na hivyo kuamua kutoa taarifa Takukuru.”
Dah!! Rushwa mbaya San