BUNGE limeelezwa kuwa watu wenye ulemavu wanabaguliwa katika kupata ajira hapa nchini kwa madai kwamba hawawezi kufanya baadhi ya kazi, anaandika Dany Tibason.
Kufuatia hali hiyo waajiri nchini wameagizwa kuzingatia sheria kila inapotokea nafasi za ajira zinazoweza kufanywa na watu hao.
Hayo yamebanishwa leo na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Antony Mavunde alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Bububu (CCM), Mwantakaje Haji Juma.
Katika swali lake, Mbunge huyo alitaka kujua ni lini serikali itatunga sheria itakayozilazimisha taasisi za serikali kutenga nafasi maalum za ajira kwa watu wenye ulemavu ili na wao wasiendelee kujisikia wategemezi katika jamii.
Akijibu swali hilo, Mavunde alisema serikali imeendelee kusimamia utekelezaji wa sheria ya watu wenye ulemavu namba 9 ya mwaka 2010 kwa kuziagiza taasisi za serikali na binafsi kuajiri watu hao wenye sifa sawia kila inapohitajika.
“Tumeendelea kufanya ukaguzi kwa kuwatumia maofisa kazi ili kuhakikisha kuwa utekelezaji wa sheria hii unafanyika ipasavyo,”alisema Mavunde.
Aidha, alisema serikali imeendelea kusimamia upatikanaji wa ujuzi na sifa linganifu kwa watu hao ili waweze kuajirika na kujiajiri kiurahisi kwa kutoa mafunzo kupitia vyuo vya ufundi, vyuo vingine kwa ujumla.
Naibu Waziri Mavunde alisema serikali imefanya jitihada za kutunga sera ya taifa ya maendeleo, haki na heshima kwa watu wenye ulemavu.
Leave a comment