MKUU wa Wilaya ya Arusha, Gabriel Daqqaro ameagiza walimu wakuu wa shule za sekondari kufundisha vipindi mbalimbali vya masomo ili kupunguza mrundikano wa vipindi kwa walimu wa kawaida, anaandika Mwandishi Wetu.
Aidha, amesisitiza kuwa wanafunzi wa vidato vya awali hadi cha tatu wanatakiwa kununua madaftari ili walimu waweze kuwapa mazoezi ya mara kwa mara.
Daqqaro aliyasema hayo Jijini hapa wakati alipokuwa akizungumza na walimu wakuu wa shule mbalimbali za Jiji la Arusha katika mkakati wa Jiji kuinua viwango vya ufaulu kwa wanafunzi wa shule za sekondari.
Alisema baadhi ya walimu wakuu hawafundishi vipindi darasani hali inayosababisha walimu wa kawaida kuelemewa na ratiba ya vipindi kwa kila darasa.
Alisema ni vyema sasa walimu wakuu hao wakaanza kufundisha darasani ili kuongeza ari ya kujua uelewa wa wanafunzi wao na kufanya mitihani ya mara kwa mara ili kubaini masomo wanayofeli.
“Walimu wakuu ni lazima sasa mfundishe vipindi naddarasani na si kukaa tu huku mkiwapangia walimu wengine vipindi lakini pia hata kama vitabu hakuna ni vyema mkaandaa utaratibu wa kuwa na klabu za wanafunzi ili waende mkataba kusoma, “alisema
Naye Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Athumani Kihamia alitoa rai kwa walimu hao kufundisha kwa bidiii na kujua tabia za wanafunzi ili waweze kufaulu huku akisisitiza kuwa ni aibu Jiji la Arusha kushika nafasi ya sita kati ya nafasi saba katika mtihani wa majaribio wa moko mwaka huu kidato cha nne.
Leave a comment