AFISA kilimo wa mkoa wa Dodoma, Benard Abraham amewataka wakulima kuwasiliana na maofisa ugani pale wanapoona mimea yao au mazao inashambuliwa na wadudu. Anaripoti Dany Tibason … (endelea).
Ofisa huyo alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na Tanzania baada ya wakulima wa mahindi wa Kibaigwa wilayani Kongwa mkoani Dodoma kulalamikia mahindi yao kushambuliwa na wadudu.
Mmoja wa wakulima wa Mahindi wilayani Kongwa, Machite Mgulambwa amesema zaidi ya heka 50 za mahindi zimeharibiwa.
Amesema licha ya kujibidisha katika kilimo na mvua kunyesha vizuri lakini wadudu wamevamia mahindi na kuyaharibu na kuwasababishia hasara kubwa wakulima.
“Tunaomba serikali iwahimize wataalamu wa kilimo kuwatembelea mara kwa mara wakulima ili kubaini changamoto wanazokumbana nazo.
“Wataalamu wa kilimo wasiwe watu wa kukaa maofisini badala yake waende mashambani kwa lengo la kuwasaidia wakulima ili waweze kulima kilimo chenye tija badala ya kilimo cha mazoea,” amesema Machite.
Mbali na hilo amesema kuwa kama serikali haitawahimiza wataalamu wa kilimo kuwa karibu na wakulima ni wazi hata sera ya Tanzania ya viwanda itakuwa ndoto.
Akizungumzia malalamiko hayo ofisa kilimo wa Mkoa, Benard Abrahamu amesema serikali imepeleka maofisa kilimo kuanzia ngazi ya kijiji.
Amesema wakulima wanatakiwa kuwasiliana na maofisa kilimo mara kwa mara pale wanapoona mimea yao au mazao pale yanapokuwa na dalili tofauti ambayo inatia shaka.
Amesema yeye kwa ngazi ya mkoa wanatakiwa kupata taarifa za mara kwa mara ili kukabiliana na matatizo na changamoto zinazowakumba wakulima.
Leave a comment