WAKAZI wa jiji la Dar es Salaam wamejitokeza kwa wingi katika vituo mbalimbali vya kuchangia damu salama, kwa lengo kuongezewa katika benki ya damu Tanzania, anaandika Jasmin Seif.
Zoezi hilo lililofanyika katika vituo vya Damu Salama Mnazi Mmoja, Hospitali ya Muhimbili, Karume, Hospitali ya Amana, Hospitali ya Mwananyamala, Hospitali ya Lugalo na Hospitali ya Sinza Palestina.
Wakazi hao wameonesha kuguswa na tukio hilo kutokana na matukio yaliyowatokea baadhi yao huku wengine wakiwa wameondokewa na ndugu, jamaa na marafiki kutokana na ukosefu wa damu mahospitalini.
Asha Saidi mkazi wa Buguruni ni miongoni mwa wakazi waliojitokeza kuchangia damu huku wakiwa wameguswa moja kwa moja na athari za ukosefu wa damu mahospitalini.
“Leo nimejitokeza kuja kutoa damu huku nikiwa na uchungu mkubwa sana, kwani mwaka jana nimepoteza mtoto wangu katika hospitali ya Amana kwa kukosa damu,” amesema Asha Said.
Mbali ya watu kuchangia damu, wengine walijitokeza kutoa misaada kwa waliokuwa wanachangia damu kama maji, juisi, matunda na biskuti kwa ajili ya waliojitolea damu.
Leave a comment