MSANII wa ‘Hip Hop’ Webiro Wakazi Wasira, maarufu kama Wakazi, ametangaza nia ya Kugombea Ubunge katika Jimbo la Ukonga, kupitia chama cha ACT-Wazalendo, kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wakazi ametangaza nia hiyo leo Jumamosi tarehe 20 Juni 2020, katika hafla ya viongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, kuwapokea wabunge 21 wa Chama cha Wananchi (CUF), jijini Dar es Salaam.
Msanii huyo wa Hip Hop amesema, adhma yake hiyo imetokana na kiu yake ya kuwaletea maendeleo na mabadiliko wananchi wa Jimbo la Ukonga.
Pia, Mwanaharakati huyo amesema hatua yake imetokana na ushawishi kutoka kwa wasanii na mashabiki wake, ambao walimshauri agombee ubunge kwenye jimbo hilo.
“Kutokana na msukumo na ushawishi wa vijana, wasanii na mashabiki wangu na nia yangu ya kuona mabadiliko na maendeleo ya taifa langu na jimbola Ukonga, nitumie nafasi hii kutangaza nia ya kuwania nafasi ya uongozi Ukonga kupitia ACT-Wazalendo,” amesema Wakazi.
Kwa mujibu wa Maalim Seif Shariff Hamad, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, kesho Jumapili tarehe 21 Juni 2020, Kamati Kuu ya chama hicho itaketi jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya kuandaa utaratibu wa uchukuaji fomu za wagombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi huo.
Baada ya kamati hiyo kuketi kesho, Jumatatu ya tarehe 22 Juni 2020, Zitto Kabwe, Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo, tatoa ratiba rasmi ya mchakato wa uchaguzi ndani ya chama hicho.
Leave a comment