JUMUIYA ya Wanawake wa dini ya Kiislamu (JUAKITA) mkoa wa Dodoma, imesema moja ya mkakati wake wa kuepukana na ugonjwa hatari wa maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19) ni pamoja na kuwafikia wajane na wasiojiweza kuwapatia misaada mbalimbali wakiwa majumbani. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Maelekezo hayo yalitolewa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Mkoa wa Dodoma, Shamim Daudi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jana Alhamisi tarehe 14 Mei, 2020 wakati wa utoaji wa misaada mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia wajane na wasiojiweza iliyofanyika baada ya kuwatembelea kwenye mitaa yao wanayoishi ikiwemo Nkuhungu, Arport, Ndachi, Chang’ombe na Mbwanga jijini Dodoma.
Shamim alisema mkakati huo ni kwa ajili ya kuwalinda na maambukizi ya virusi vya Corona pamoja na kuwaondolea matembezi yasiyo lazima wanayoyafanya kwa ajili ya kutafuta kipato cha kujikimu.
Alisema jumuiya hiyo ya wanawake imeamua hivyo kwa kuwafikia kila mmoja wapo wakiwa majumbani mwao pia pamoja na kutekeleza agizo toka kwa viongozi wa serikali na dini ili kuhakikisha ugonjwa huo unadhibitiwa kwa kila njia.
“Serikali na viongozi wetu wa dini wamekuwa wakihamasisha njia mbalimbali za kujilinda na ugonjwa huo moja wapo ni kuepukana na matembezi yasiyo lazima,hivyo ili kuwafanya wajane na wasiojiweza wasitoke hivyo majumbani sisi Juakita tumeamua kuwafuata majumbani na kuwapatia misaada mbalimbali kwa vitendo,” alisema.
Mwenyekiti huyo alisema jumuiya hiyo ambayo pia ipo chini ya Bakwata, imekuwa ikitoe elimu kwenye makundi mbalimbali juu ya madhara ya ugonjwa huo kwa vitendo ili watu waweze kujiepusha na janga hili.
Katika hatua nyingine, mwenyekiti huyo aliwasihi watu taasisi na mashirika kujitoa kwa moyo kwa ajili ya kusaidia makundi hayo yanayokabiliana na changamoto mbalimbali za kimaisha.
Akizungumza wakati wa ugawaji huo uliofanyika katika maeneo mbalimbali wakiwa majumbani mwao misaada iliyotolewa kwa wajane na wasiojiweza ni pamoja na unga wa kula, mchele, maharage, sukari, tambi, chumvi na mafuta ya kupikia.
Kwa upande wake, Shekhe wa Mkoa wa Dodoma, Alhaji Mustaph Rajabu aliwataka wajane kuheshimu utaratibu huo utakaotumika wa kuwafuata majumbani wa kuletewa misaada kwa kuwa, itawasaidia kutotembea mwendo mrefu kutafuta mahitaji ikiwa ni pamoja na kujiepusha na misongamano ambayo inaweza kuwapatia maambukizi ya virusi vya Corona.
Aidha, aliwataka kujihadhali pia wanapokuwa majumbani mwao kwa kuhakikisha wananawa kwa maji chirizika na sabuni kuvaa barakoa, ili kujilinda na janga hili la ugonjwa wa Covid 19.
Leave a comment