WATU watatu wameuawa huku 50 wakitafuta hifadhi kwenye vituo vya polisi katika mashambulizi yaliyofanywa na baadhi ya raia wa Afrika Kusini, wanaopinga uwepo wa wageni nchini humo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Tukio hilo la kusikitisha limetokea leo tarehe 1 Aprili 2019 mjini Durban nchini Afrika Kusini, baada ya raia hao kuvamia maeneo ya biashara ya wageni ikiwemo maduka na kuanzisha fujo, sambamba na kuharibu mali, wakishinikiza wageni kuondoka nchini mwao.
Waziri wa Masuala ya Kigeni nchini Afrika Kusini, Lindiwe Sisulu amelaani matukio hayo akisema kwamba, hayakubaliki na kuitisha mkutano wa dharura na mabalozi wa nchi za kigeni nchini humo kwa ajili ya kujadili kadhia hiyo.
Aidha, Sisulu amewaagiza maafisa wa polisi kuwadhibiti watu wanaoshambulia wageni.
Fujo hizo zilianza jana Jumapili tarehe 31 Machi 2019 ambapo watu takribani 100 walishambuliwa pamoja na maduka kadhaa kuharibiwa
Mwishoni mwa wiki iliyopita katika mitandao ya kijamii ulisambaa waraka unaodaiwa kutoka kwa kundi la raia wa Afrika Kusini wanaopinga wageni kufanya shughuli za kibiashara pamoja na ajira nchini mwao, wakidai kuwa haiwezekani wao wakose ajira wakati wageni wanazo.
Leave a comment