JUKWAA la Wahariri Tanzania (TEF) limewataka wanasiasa nchini humo kutokutoa matamshi ya kuwachochea wananchi kujenga chuki dhidi ya wanahabari na vyombo vya habari hususani kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea
Kauli hiyo imetolewa jana Jumapili tarehe 23 Augost 2020 jijini Dodoma na Kaimu Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati akihitimisha mkutano mkuu wa wahariri.
Balile alisema, wanasiasa wanatakiwa kuchunga kauli zao pindi wanapokuwa katika mikutano yao ya kisiasa na zaidi wajikite kunadi sera zao na kuwaelezea wananchi watafanya nini pindi watakapopewa ridhaa ya kuongoza.
“Jukwaa limelazimika kutoa tamko hilo kutokana na kauli iliyotolewa hivi karibuni na aliyekuwa mbunge wa jimbo la Iringa Mjini kupitia Chadema, Mchungaji Peter Msigwa kwa kuwahamasisha wananchi kuwapuuza waandishi na vyombo vya habari.”
“Hivi karibuni kuna taarifa inatembea katika mitandao ya kijamii ikieleza Mchungaji Msigwa aliwahamasisha wanachama wa Chadema kuwa wawapuuze waandishi wa habari na vyombo vya habari kwa kuwa waandishi walisusa kuandika habari za Chadema wakati alipokuwepo mgombea urais wa Chadema Tundu Lissu wakati akitafuta wadhamini.”
Balile alisema, “kauli kama hizo zinaweza kusababisha chuki kwa wananchi na kama hatutakemea kauli hizo kuna siku viongozi wa siasa wanaweza kuhamasisha waandishi wapigwe na wakapigwa.
“Kwa maana hiyo, Jukwaa hatukatai waandishi wawe sehemu ya kupigwa kwani waandishi hawana vyama na wanatakiwa kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria na utaratibu kwa lengo la kuwahabarisha watu wote” amesema Balile.
Hata hivyo, Balile aliviasa vyama vya siasa kushirikiana na waandishi wa habari kwa kuwapa ratiba au taarifa pale wanapokuwa wakifanya mikutano kwani waandishi hawawezi kuwa wanatambua kinachofanyika kila mara kwakuwa wanahabari siyo wanasiasa.
Pamoja na mambo mengine, Balile alisema, taaluma ya habari ni mhimiri wanne hiyo imethibitika katika kipindi chote cha ugonjwa wa Corona nchi ilikuwa ikiendeshwa na vyombo vya habari kwa kutoa elimu kwa jamii kwani kila mtu alikuwa akitumia vyombo vya habari na jamii iliweza kupata elimu hasa kutumia vifaa vilivyokuwa vikitakiwa kama vile vitakasa mikono na utumiaji wa maji tiririka.
Aidha Kiongozi huyo alisema, vyombo vya habari nchini vinatakiwa kuzingatia kanuni, sheria, miongozo na maadili ya uandishi wa habari na kukataa kutumiwa na wanasiasa wenye ajenda zao binafsi ambazo hazina misingi ya Taifa.
“Tunapoelekea katika uchaguzi mkuu, wanahabari tuhakikishe tunaitumia nguvu hiyo kwa uangalifu ili kuweza kujenga taifa letu kwa maana ya kwamba sisi hatuna nchi nyingine zaidi ya Tanzania” alisema Balile.
Leave a comment