PAMOJA na jitihada zinazofanywa na serikali, katika kuzuia uhalifu unaofanywa na baadhi ya waendesha bodaboda na bajaji, bado kundi hilo limeendelea kuwa tishio jijini Dar es Salaam, anaandika Dany Tibason.
Hata serikali kupitia Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba, imekiri kwamba kuna ongezeko la uhalifu unaofanywa na waendesha vyombo hivyo vya usafiri, katika maeneo mengi ya Jiji hilo.
“Tunachukua hatua mbalimbali kukabiliana na uhalifu huo, ikiwa ni pamoja na kufanya doria za magari, pikipiki na miguu, kuanzisha na kushirikiana na vikosi vya ulinzi shirikishi ili kubaini na kuzia uhalifu katika maendo ya makazi,” ameeleza Mwigulu.
Maelezo hayo yalitolewa wakati wa kipindi cha maswali na majibu, baada ya Mbunge wa Viti Maalum, Hawa waifunga (Chadema), kutaka kujua hatua zilizochukuliwa na serikali, kudhibiti wimbi la uhalifu, ambalo alisema ni tishio kwa watumiaji wa vyombo hivyo vya usafiri.
“Je, serikali ina utaratibu gani wa kuhakikisha na kutambua mmiliki, dereva na mahali zinapopaki bajaji na bodaboda?,” alihoji Mwaifunga.
Akijibu, Waziri Nchemba, alisema kupitia Serikali za mitaa na halmashauri za Jiji la Dar es Salaam, unafanyika uhakiki wa pikipiki hizo ikiwa ni pamoja na kuwapangia maeneo ya kupaki ambako ni lazima zijisajili ili dereva na mmiliki wafahamike .
Leave a comment