MAHAKAMA imewaachia huru wafuasi saba wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kuwapa dhamana wanachama watatu wenye majeraha ya risasi baada ya kufyatuliwa risasi na Polisi kwenye maandamano. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Maandamano hayo yalifanyika Februali 16 mwaka huu, ambapo wafuasi wa Chadema waliandamana kwenda kwenye Ofisi za Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni kudai nakala ya hati za viapo za Mawakala wa chama hicho.
Wanachana wa Chadema waliokuwa rumande huku wakiwa na majeraha ya risasi na kuachiwa kwa dhamana na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ni Aida Olomi, Erick John na Isack Ng’aga.
Wafuasi hao watatu ambao waliwasili mahakamani wakiwa na majeraha yao ya risasi, walipandishwa kizimbani na kusomowa shtaka la kufanya mkusanyiko kinyume na sheria na waliunganishwa kwenye mashtaka na watuhumiwa wengine 28.
Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa, wakili wa Serikali, Patrick Mwita amewasomea mashtaka watuhumiwa hao kwamba watuhumiwa hao na wengine 28 watakaonganishwa nao Machi 8, mwaka huu kwa pamoja, Februali 16, 2018 wakiwa eneo Mkwajuni, Kinondoni, jijini Dar es Salaam walifanya mkusanyiko kinyume na sheria.
Mwita alidai kuwa mkusanyiko huo ulilenga kufanya uvunjifu wa amani na kusababisha taharuki, watuhumiwa hao walikana mashtaka hayo. Wameachiwa kwa dhamana yenye mdhamini mmoja alisaini bondi ya Sh. 1.5 Milioni.
Upande wa mashtaka umedai kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika, hivyo kesi hiyo itatajwa tena Machi 8, mwaka huu.
Wakati huohuo, Mahakamani hapo watuhumiwa saba ambao ni wafuasi wa Chadema waliachiwa huru baada ya upande wa mashataka kushindwa kuthibisha mashtaka yao.
Watuhumiwa hao Sundy Urio, Kizito Damia, Joseph Samky, Chrisant Clemence, Wilfred Ngowi, Karim Ally na Kinyaiya Siriri walipandishwa kizimbani kwa kosa la kuwarushia mawe askari Polisi walipokuwa kwenye majukumu yao.
Walikuwa wanakabiliwa na kesi ya kufanya fujo ambapo inadaiwa Januari 6, 2015 waliwapiga mawe Polisi na kuwazuia kutekeleza majukumu yao maeneo ya Ubungo Riverside.
Thomas Simba Hakimu Mkazi mkuu wa Mahakama hiyo baada ya kupitia ushahidi wa Jamhuri amesema kuwa ushahidi huo ni dhaifu hauwezi kuwatia hatiani watuhumiwa hao.
Leave a comment