SHIRIKISHO la vyama vya wafanyakazi Tanzania (TCTA) Mkoa wa Dodoma, kipato cha mshahara kwa mfanyakazi kwa mwezi hakikidhi mahitaji kwa mfanyakazi, anaandika Dany Tibason.
Mbali na kipato kuwa kidogo shirikisho hilo limeitaka serikali kuongeza kima cha chini cha mshahara ili kuwafanya wafanyakazi kufanya kazi kwa moyo na kwa ufanisi wa kazi zao.
Hayo yameelzwa na Shirikisho hilo wakati Katibu wa TUCTA mkoa wa Dodoma, Ramadhani Mwendwa wakati akisoma risala kwa mgeni rasmi ambaye alikuwa awe mkuu wa mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana. Hata hivyo Rugimbana alimkaimisha mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Jabiri Shekimweli.
Katika risala hiyo Mwendwa amesema kipato cha ujira wa mshahara wa mwezi wanacholipwa wafanyakazi hakiridhishi kabisa.
Amesema malipo madogo husababisha kukosekana kwa tija mahala pa kazi kwani wafanyakazi hukosa moyo wa kujituma katika kufanya kazi na hivyo kulazimika kutumia muda wa kazi kutafuta njia nyingine kwa kujiongezea kipato.
Mwendwa amesema kama serikali ingekuwa na nia ya dhati ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi ingeweza kuwalipa vizuri kwani vipo vyanzo vingi serikalini ambavyo vingeweza kuongeza pato la taifa na kuwafanya wafanyakazi kulipwa vizuri.
Akizungumzia sekta binafsi, Mwendwa amesema sekta hizo zimekuwa bingwa kuwanyonya wafanyakazi wao kwa kutowapatia mikataba ya kazi.
“Sekta binafsi waajiri wamekuwa bingwa wa kuwanyonya wafanyakazi ikiwemo tabia ya kutofuata sheria za ajira kwa kuajiri wafanyakazi bila kuwapa mikataba ya ajira ili kutimiza dhuruma yao ikiwemo kutowachangia kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii na kukwepa kodi ya malipo ya payee,” amesema Mwendwa.
Akizungumzia kuhusu madeni sugu, Mwendwa ameitaka serikali kulipa madeni yote sugu kwa kada zote ili kuondoa maumivu ya muda mrefu ambayo inawaumiza wafanyakazi.
Amesema kwamba licha ya serikali kulipa baadhi ya malimbikizo lakini bado haijaweza kulipa kwa kada zote na badala yake wamekuwa wakishindwa kulipa madeni hayo ambayo kwa sasa ni sugu na yanawaumiza wafanyakazi pasipokuwa na sababu.
Aidha ameitaka serikali kutotumia makosa ya baadhi ya watu walioshindwa kutawala walioshindwa kusimamia majukumu yao ya kiutawala kwa kuwaadhibu watu wasiokuwa na hatia.
Amesema licha ya serikali kutoa punguzo kutoka asilimia 11 hadi asilimia 9 lakini bado wafanyakazi wanaiomba serikali kupunguza kodi hiyo kwa wafanyakazi wengine kwani punguzo hilo limefanyika kwa wafanyakazi wachache wanaolipwa kima cha chini lakini kodi kubwa hadi asilimia 30 inaendelea kukatwa kwa wafanyakazi wenye mishahara mikubwa kana kwamba wanaadhibiwa kwa kulipwa mishahara mikubwa.
Akijibu risala hiyo mku wa wilaya ya Mpwapwa kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana, Jabiri Shekimwel amesema serikali inaandaa utaratibu wa kuboresha mishahara ya watumishi wa Umma baada ya kukamilisha zoezi zima la uhakiki wa vyati.
Leave a comment