KAMATI ya Katiba na Sheria ya Bunge la Jamhuri, leo imeanza rasmi kupokea maoni ya wadau juu ya muswada wa sheria vya vyama siasa Na. 4 wa mwaka 2018, mjini Dodoma. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza mbele ya kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria, Jeremia Mtobyesa, mwakilishi kutoka chama cha wanasheria Tanganyika (TLS), ameliambia Bunge kuwa sheria inayotungwa “imesheheni vimelea ya udikteta.”
Amesema, baadhi ya vifungu vilivyomo kwenye muswada vinapingana na katiba ya nchi. Ametoa mfano wa kifungu kinachotoa kinga kwa msajili wa vyama na vile vinavyozuia watu kukata rufaa.
Mtobyesa amesema kuwa katika taifa hili, kila taasisi kumewekwa utaratibu wa kukata rufaa. Akaongeza,”kutoruhusu ukataji wa rufaa kama ambavyo sheria inayotungwa inavyotaka, ni kinyume na katiba.”
Naye Soba Sang’anya, wakili wa mahakama kuu, akizungumzia kinga inayotolewa kwa msajili wa vyama amesema kuwa utoaji wa kinga hiyo unaweza kusababisha watu wengine kuomba kinga hiyo.
“Kuna watu wengi wanaofanya kazi kama msajili wa vyama. Hawana kinga. Lakini hapa tunataka kutoa kinga kwa mtu ambaye hata kupigiwa kura, hajapigiwa. Kwa sababu, hili likiachwa kama lilivyo, watu wengine wanaweza kuomba kinga ya aina hiyo,” ameeleza Sang’anya.
Baadhi ya wajumbe waliochangia maoni yaliyowasilishwa na wadau walihoji uelewa wao katika muswada. Hilo lilitokana na baadhi ya wasilishaji wa maoni, kushindwa kufanya uchambuzi. Badala yake, wakaishia kunakiri muswada ulioletwa.
Leave a comment