SERIKALI jijini Nairobi, imetangaza kuongezeka wagonjwa 25 wa visa vya karibuni vya maambukizi ya Corona, kwatu tisa. Kati yao, saba ni raia wa Kenya na wawili wakiwa ni wageni. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Waziri wa Afya nchini humo, Mutahi Kagwe amesema, juhudi za kuwatafuta watu wengine 745 waliotangamana na visa vya hivi karibuni zinaendelea.
Waziri huyo amesema, wagonjwa wametengwa na wanafuatiliwa kwa karibu. Wagonjwa hao wa coronavirus wamethibitishwa katika mji wa Nairobi, na kaunti za Mombasa, Kilifi na Kwale.
Amesema kuwa serikali itafanya vipimo vya lazima kwa wasafiri na wale watakaokuwa wameongozana na wagonjwa hao.
Amesema, “…inasikitisha kwamba baadhi ya Wakenya wanapuuza maagizo tuliyoweka kukabiliana na ugonjwa huu.”
Akihutubia vyombo vya habari Juampili iliyopita, Bwana Kagwe alisisitiza umuhimu wa raia wa Kenya kuzingatia hatua zilizowekwa ili kuepusha maafa.
Alisema, “huu ugonjwa sio mzaha” na kuongeza, “wiki mbili zijazo zitakuwa hatari zaidi endapo hali ya maambukizi haitadhibitiwa.”
Taarifa zinasema, hatua za dharura zilizochukuliwa kuanzia usiku wa Jumapili, baa zote zitafungwa na wenye hoteli wataruhusiwa kuuza chakula cha kwenda kula nyumbani.
Ibada za Kanisa na Swala za pamoja Misikitini zimesitishwa huku mazishi ikiruhusiwa kuhudhuriwa na familia ya marehemu pekee. Sherehe za harusi pia zimepigwa marufuku.
Hyao ni masharti makali kuwekwa na mamlaka ya Kenya tangu ilipotangaza kisa cha kwanza cha coronavirus nchini humo 13 Machi mwaka huu.
Huku hayo yakijiri serikali imetangaza kuwa itamfikisha mahakamani naibu wa gavana wa jimbo la Kilifi Pwani ya Kenya kwa kukaidi maagizo ya kujiweka karantini binafsi baada ya kuwasili nchini wiki iliyopita.
Kwa sasa anazuiliwa katika kituo cha serikali cha kuwatenga watu walio na ugonjwa wa corona.
Leave a comment