VYAMA vya upinzani vilivyojitoa katika kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, vimepewa nafasi 163 kati ya 332,160, zilizokuwa zinashindaniwa katika uchaguzi huo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 25 Novemba 2019 jijini Dodoma, Selemani Jafo, Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, amesema vyama vya upinzani ikiwemo vilivyojitoa kushiriki kwenye uchaguzi huo, vimeambulia wenyeviti katika vijiji, vitongoji , wajumbe kundi la wanawake na mchanganyiko.
Jafo amefafanua kuwa, Chadema haikufanikiwa kupata mtaa, lakini imepata mwenyekiti wa kijiji mmoja, wa vitongoji 19, kundi la wanawake 39 na mchanganyiko 71.
Wakati CUF kikipata mwenyekiti wa kijiji mmoja, vitongoji viwili, wajumbe kundi la wanawake watatu na mchanganyiko 14.
Huku ACT-Wazalendo, kikipata mwenyekiti wa kitongoji mmoja, mjumbe mmoja kundi la wanawake na wajumbe 11 mchanganyiko.
Jafo amesema Chama cha Mapinduzi (CCM) kimepata wenyeviti wa vijiji 12,260 kati ya 12,262, pamoja na mitaa yote 4,263 sawa na asilimia 100.
Pia, imepata wenyeviti wa vitongoji 63,970 kati ya 63,992, wajumbe kundi la wanawake 106,577 kati ya 106,622 na wenyeviti mchanganyiko 144,925 kati ya 145,021.
“Matokeo ya ujumla kwa wagombea kwa kila chama katika mchakato wa uchaguzi, nafasi ni 332,160 zilihusika katika uchaguzi. Vijiji 12,262, mitaa 4,263, vitongoji 63,992, wajumbe kundi la wanawake 106,622, kundi mchanganyiko 145,021,” ameeleza Jafo na kuongeza;
“Matokeo ya CCM waliopita bila kupingwa na kupigiwa kura, vijiji 12,260 sawa na asilimia 99.9, upande wa mitaa 4,263 sawa na 100%, kitongoji 63,970 99.4% , kundi la wanawake 106,577 sawa na 99.66%, wajumbe mchanganyiko 144,925 sawa 99.6%.”
Kwa upande wa vyama vilivyoshiriki uchaguzi huo, UDP kimepata nafasi moja ya mjumbe katika kundi la wanawake na DP kimepata sawa na UDP.
Leave a comment