MKUTANO wa Kamati ya Fedha na Uongozi wa halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, umemalizika baada ya kufanyika chini ya mtutu wa bunduki. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
“Mkutano ule ulikuwa uanze saa 8 mchana, lakini umeanza saa 12 na dakika tano Arasili. Na hapa ni baada ya mkurugenzi kuita polisi na kuendesha kikao kwa njia ya mtutu wa bunduki,” ameeleza Saed Kubenea, mbunge wa Ubungo na mjumbe wa Kamati ya Fedha katika Jiji la Dar es Salaam.
Amesema, “…hivi vinavyoendeshwa hapa haviwezi kuwa vikao vya Jiji kwa mujibu wa kanuni zetu. Vikao vinatakiwa viendeshwe kwa uhuru na kila mjumbe atakuwa na uhuru wa kutoa mawazo yake bila kuingilia. Linapokuja suala la Polisi kusimamia vikao, hapo hakuna mkutano.”
Kubenea amesema hayo mara baada ya kutoka kwenye kikao hicho ambapo ameleeza kuwa vikao vya aina hiyo, “vimekosa uhalali.”
Amemtuhumu mkuregenzi wa jiji hilo kwa kushindwa kuwa mtumishi wa umma, badala yake ameamua kujiegemeza kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Kwa mujibu wa Kubenea, kitendo cha kuita Polisi kinahatarisha mustakabali wa Jiji hilo na kwamba “vikao vya Jiji kuendeshwa na mtutu wa bunduki, ni hatari kwa mustakabali kwa Jiji.”
Amesema, msimamo wake yeye na wenzake, ni kuwa Isaya Mwita ni meya halali wa Jiji na wanaomtaka kumtoa kwenye nafasi hiyo, wafuate taratibu.
MwanaHALISI Online limeshindwa kumpata mkurugenzi wa Jiji, Sipora Liana, kutoa ufafanuzi wa madai hayo.
Naye Patrick Assenga, diwani wa Kata ya Tabata na Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu ya jiji hilo amesema, kikao kilichofanyika kimetia aibu halmashauri hiyo.
Leave a comment