CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimeeleza kwamba, kinashughulikia agizo la Halmashauri Kuu yake ya Taifa, la kuwahoji makatibu wakuu wastaafu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana na Yusuph Makamba, pamoja na Bernad Membe, Waziri Mstaafu wa Mambo ya Nje. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM, mwezi mmoja baada ya halmashuari kuu ya chama hicho, kuagiza vigogo hao wahojiwe katika Kamati ya Usalama na Maadili ya Taifa, ili wajibu tuhuma za kimaadili zinazowakabili.
Polepole amesema suala hilo linashughulikiwa kwa kufuata taratibu husika, kisha umma utajulishwa kuhusu hatma ya suala hilo.
“Jambo la usalama na maadili litafanyiwa kazi kwenye ngazi ya kamati hiyo, kisha litakwenda kwenye Kamati Kuu na baadaye Halmashauri Kuu, kisha baada ya hapo umma unajulishwa,” ameeleza Polepole.
Kauli hiyo imekuja kufuatia watuhumiwa hao, kuweka bayana kwamba wanasubiri kwa hamu wito wa kwenda kuhojiwa.
Jana tarehe 15 Januari 2020, kupitia ukurasa wake wa Twitter, Membe amezungumzia sakata hilo akiandika kwamba, wahusika bado wanakusanya nguvu na ujasiri wa kuwahoji.
“Nadhani watatuita wakati muafaka. Wanakusanya nguvu na ujasiri,” ameandika Membe.
😅😅😅😅 Nadhani watatuita wakati muafaka. Wanakusanya nguvu na ujasiri.
— Bernard K. Membe (@BenMembe) January 14, 2020
Hivi karibuni Makamba alizungumzia sakata hilo, na kusema kuwa, kama atapokea barua ya wito kwenda kwenye kamati hiyo, hatokawia kwenda.
Viongozi hao wanakabiliwa na tuhuma za kukiuka maadili ya chama hicho, baada ya sauti zinazodaiwa kuwa za kwao, zenye mazungumzo yanayokosa utendaji wa uongozi uliopo madarakani, kuvuja mitandaoni.
Membe, Kinana na Makamba ni miongoni mwa vigogo wa CCM, waliohusishwa moja kwa moja katika sakata hilo la kuvuja kwa sauti hizo.
Wengine walikuwa ni Nape Nnauye, Mbunge wa Mtama, January Makamba, Mbunge wa Bumbuli na William Ngereja, Mbunge wa Sengerema, ambao waliomuomba msamaha Rais Magufuli, na msamaha wao kuridhiwa na Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM.
Sakata hilo liliibuka baada ya Kinana na Makamba, kuandika waraka unaokosoa ukimya wa serikali katika kushughulikia watu wanao wachafua wastaafu nchini.
Leave a comment