WATU 40 wameuawa na kujeruhiwa katika mapigano mapya yaliyotokea katika jimbo la Yei nchini Sudan Kusini, anaandika Hellen Sisya.
Mapigano hayo ambayo yanatokana na mgogoro wa kisiasa nchini humo, yametokea kati ya jeshi la nchi hiyo pamoja na waasi wa taifa hilo.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mpaka sasa watu wengi wameuawa na kujeruhiwa katika vita vinavyoendelea nchini humo na umezitaka pande kuu hasimu katika mgogoro huo kufanya juhudi za kurejesha amani na maridhiano.
Sudan Kusini ilitumbukia katika machafuko na mapigano kati ya wafuasi wa Rais Salva Kiir na makamu wake wa zamani Riek Machar tangu mwaka 2013.
Salva Kiir alimtuhumu makamu wake huyo kwamba alipanga njama za kufanya mapinduzi.
Baada ya kushamiri kwa mgogoro huo na kwa juhudi mbalimbali za kimataifa mwaka 2015 pande hizo mbili zilifikia makubaliano ya kugawana madaraka.
Hata hivyo, kukiukwa kwa vipengele vya makubaliano hayo, kulipelekea kuvunjika kwa makubaliano hayo na kwa mara nyingine nchi hiyo changa zaidi barani Afrika ikatumbukia katika vita na machafuko.
Leave a comment